Hamia kwenye habari

Walivaa Pembe Tatu ya Zambarau

Walivaa Pembe Tatu ya Zambarau

Maud anaishi nchini Ufaransa na anafanya kazi katika shule ambapo anawasaidia watoto walemavu wanapokuwa darasani. Hivi karibuni wanafunzi katika darasa moja walikuwa wakijifunza kuhusu Yale Maangamizi Makubwa na kambi za mateso za Wanazi. Wafungwa katika kambi hizo walikuwa na kitambaa chenye rangi kilichoshonwa kwenye sare zao. Rangi na umbo la kitambaa hicho ilionyesha sababu ya mtu huyo kufungwa.

Mwalimu alisema hivi aliporejelea vitambaa vya pembe tatu ya zambarau vilivyovaliwa na wafungwa fulani: “Nafikiri ilikuwa kwa sababu walikuwa watu wanaolala na watu wa jinsia yao.” Baada ya darasa, Maud alizungumza na mwalimu na kumweleza kwamba Wanazi walitumia pembe tatu ya zambarau kuwatambulisha Mashahidi wa Yehova. a Alimwambia kwamba anaweza kumletea habari fulani kuhusu hilo. Mwalimu alikubali na akamwomba Maud ashiriki habari hizo pamoja na wanafunzi wengine.

Wakati wa darasa lingine, mwalimu mwingine alitumia chati iliyoonyesha ishara mbalimbali zilizovaliwa na wafungwa. Chati hiyo ilionyesha waziwazi kwamba pembe tatu ya zambarau iliwatambulisha Mashahidi wa Yehova. Baada ya darasa, Maud alimpa mwalimu huyo habari kuhusu jambo hilo. Mwalimu alikubali na kufanya mipango ili Maud azungumze mbele ya wanafunzi.

Maud akiwa ameshika machapisho aliyotumia

Maud alitayarisha sehemu ya dakika 15 kwa ajili ya darasa la kwanza, lakini muda wa kuzungumza ulipofika aliambiwa: “Utazungumza kwa saa nzima.” Maud alianza kwa kuonyesha video iliyosimulia kuhusu mateso ambayo Mashahidi wa Yehova walikabili chini ya Wanazi. Simulizi hilo liliposema kwamba Wanazi waliwachukua watoto 800 kutoka kwa wazazi wao Mashahidi, Maud alisimamisha video na kusoma masimulizi kuwahusu watoto watatu kati ya hao. Baada ya kuonyesha video yote, Maud alimalizia kwa kusoma barua ya kuaga iliyoandikwa mwaka wa 1940 na Gerhard Steinacher, Shahidi kutoka Austria mwenye umri wa miaka 19. Aliwaandikia wazazi wake barua hiyo saa chache tu kabla ya kuuawa na Wanazi. b

Maud alitoa hotuba kama hiyo katika darasa la pili pia. Kwa sababu ya ujasiri wa Maud, walimu wote wawili sasa wanahakikisha kwamba wanazungumza kuhusu Mashahidi wa Yehova wanapofundisha waathiriwa wa kambi za mateso ya Wanazi.

a Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani, waliojulikana kama Bibelforscher (Wanafunzi wa Biblia), walifungwa kwa sababu ya kukataa kuunga mkono Wanazi.

b Gerhard Steinacher alihukumiwa kifo kwa kukataa kujiunga na jeshi la Ujerumani. Katika barua yake ya kuaga, aliandika hivi: “Ningali mtoto. Nitasimama imara ikiwa tu Bwana atanipa nguvu, na ninasali anipe nguvu.” Asubuhi iliyofuata Gerhard aliuawa. Maneno yaliyoandikwa kwenye kaburi lake yalisema hivi: “Alikufa kwa sababu ya kumheshimu Mungu.”