Hamia kwenye habari

Makasisi Wenye Hasira Watendewa kwa Upole

Makasisi Wenye Hasira Watendewa kwa Upole

Artur, mwangalizi wa mzunguko nchini Armenia, alikuwa akitembelea kutaniko la Mashahidi wa Yehova. Aligundua kwamba hawakuwa wamewahi kushiriki utumishi wa hadharani, ambao unahusisha kutumia vigari vyenye machapisho ya Biblia. Ili kuwatia moyo wenyeji washiriki utumishi huo, Artur na mkewe, Anna, pamoja na Shahidi anayeitwa Jirayr, walisimamisha kigari cha machapisho katika mji mdogo. Walichagua eneo ambalo watu wengi hupita.

Muda si muda, watu walianza kupendezwa na kuchukua machapisho. Hata hivyo, baada ya muda mfupi, mbinu hiyo mpya ya kuhubiri ilivuta uangalifu wa wapinzani. Makasisi wawili wakakikaribia kigari, na ghafla, mmoja wao akakipiga teke na kukiangusha. Kisha akampiga kofi Artur, na hivyo kufanya miwani yake ianguke. Artur, Anna, na Jirayr walijaribu kuwatuliza makasisi hao bila mafanikio. Makasisi hao walikanyanga-kanyaga kigari na kutawanya machapisho. Baada ya kuwatukana na kuwatisha Mashahidi, wakaondoka.

Artur, Anna, na Jirayr walienda kwenye kituo cha polisi ili kufungua mashtaka. Waliandikisha malalamiko yao na kuzungumza kifupi kuhusu Biblia na maofisa wengi wa polisi na wafanyakazi wengine. Mashahidi hao watatu walipelekwa kwenye ofisi ya mkuu wa polisi. Mwanzoni alitaka kupata habari zaidi kuhusu malalamiko yao. Lakini aliposikia kwamba Artur, ambaye ni mtu mwenye misuli, hakupigana alipopigwa kofi, ofisa huyo aliacha kuuliza maswali kuhusu kesi hiyo na akaanza kuuliza maswali kuhusu mafundisho ya Mashahidi. Hilo lilifanya kuwe na mazungumzo ya saa nne! Ofisa huyo alipendezwa sana na kile alichosikia hivi kwamba akasema hivi kwa msisimuko: “Hiyo ni dini nzuri sana! Ningependa kujiunga nayo!”

Artur na Anna

Siku iliyofuata, Artur alifanya utumishi wa hadharani tena katika eneo lilelile, na mzee fulani aliyeona matukio ya siku iliyotangulia akamfikia. Mzee huyo alimpongeza Artur kwa kuwa mtulivu na kutolipiza kisasi. Aliongeza kusema kwamba kile alichoona kilimfanya aache kuwaheshimu makasisi hao kabisa.

Jioni hiyo ofisa mkuu alimwita Artur kwenye kituo cha polisi tena. Lakini badala ya kuzungumzia kesi yao, aliuliza maswali zaidi kuhusu Biblia. Polisi wengine walijiunga na mazungumzo hayo.

Siku iliyofuata, Artur alimtembelea tena ofisa huyo mwenye cheo cha juu, lakini pindi hii alitaka kumwonyesha video zilizotegemea Biblia. Ofisa huyo aliwaita polisi wengine watazame video hizo pamoja naye.

Kwa sababu ya mwenendo usiofaa wa makasisi hao, polisi walipata ushahidi kwa mara ya kwanza. Walipata kuwaelewa Mashahidi wa Yehova kwa njia inayofaa.