Hamia kwenye habari

Alijifunza Kutoka kwa Wafungwa

Alijifunza Kutoka kwa Wafungwa

Mwanamume fulani alikimbilia nchini Norway kama mkimbizi kutoka Eritrea mwaka 2011. Mashahidi wa Yehova walipomtembelea, alisema amewahi kukutana na Mashahidi akiwa nchini kwao. Akawaambia kwamba alipokuwa jeshini, aliona Mashahidi ambao walifungwa kwa ajili ya imani yao kwa sababu ya kukataa kulazimishwa kufanya utumishi wa kijeshi hata walipotendewa kikatili.

Mambo yalibadilika ghafla na mwanamume huyo pia akafungwa gerezani. Alipokuwa huko alijikuta akiwa na Mashahidi watatu—Paulos Eyasu, Negede Teklemariam, na Isaac Mogos—ambao wamekuwa kifungoni kwa sababu ya imani yao toka mwaka 1994.

Alipokuwa gerezani, mwanamume huyu alijionea mwenyewe kwamba Mashahidi wa Yehova wanaishi kulingana na kile wanachofundisha. Aliona jinsi walivyokuwa wanyoofu na hata walishiriki chakula chao pamoja na wafungwa wengine. Aliona jinsi wafungwa wenzake waliokuwa Mashahidi walivyojifunza Biblia pamoja kila siku na kuwakaribisha wengine wajiunge nao. Kila walipopewa nafasi ya kuachiliwa huru ikiwa tu wangetia sahihi hati ya kukana imani yao, walikataa.

Mambo hayo aliyojionea mwanamume huyu mnyoofu yalimgusa moyo sana, na baada ya kufika nchini Norway, alitaka kujua kwa nini Mashahidi wa Yehova wana imani yenye nguvu kadiri hiyo. Hivyo Mashahidi walipomtembelea, mara moja alianza kujifunza Biblia pamoja nao na kuhudhuria mikutano.

Septemba 2018, alibatizwa kama mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Sasa anatumia kila fursa anayopata kukutana na watu kutoka Eritrea na Sudan, ili awatie moyo wajifunze Biblia na wasitawishe imani yenye nguvu.