Hamia kwenye habari

Sala za Mwanamke Kipofu Zajibiwa

Sala za Mwanamke Kipofu Zajibiwa

Yanmei, dada, Shahidi kutoka Asia, alimuuliza mwanamke fulani kipofu anayeitwa Mingjie, ikiwa angependa amsaidie kuvuka barabara. a Mingjie akajibu: “Asante. Mungu akubariki!” Baada ya kuvuka, Yanmei alimuuliza Mingjie ikiwa angependa wakutane ili wazungumzie Biblia pamoja. Baadaye, Mingjie alisema kwamba alikuwa akisali kila siku ili Mungu amwongoze katika kutaniko lake la kweli. Kwa nini alikuwa akimwomba Mungu jambo hilo?

Mingjie alisema kwamba mwaka 2008 alikubali mwaliko wa kuhudhuria kanisa la watu wenye ulemavu kutoka kwa rafiki yake aliyekuwa kipofu pia. Baada ya kusikiliza mahubiri yaliyotolewa, Mingjie alimuuliza kasisi ni kitabu gani alichokuwa akitumia kunukuu maneno aliyosema. Akamwambia kwamba ilikuwa Biblia, Neno la kweli la Mungu. Mingjie alianza kutamani kusoma kitabu hicho. Kwa hiyo alipopata Biblia ya Kichina iliyo katika maandishi ya vipofu, alisoma mabuku yote 32 kwa karibu miezi sita tu. Mingjie alipoendelea kusoma Biblia aligundua kwamba fundisho la utatu, lililokuwa likifundishwa katika kanisa alilokuwa akihudhuria, ni la uwongo na kwamba Mungu ana jina, Yehova.

Baada ya muda, Mingjie alianza kuvunjwa moyo na mwenendo wa washiriki wa kanisa hilo. Aligundua kwamba hawakuwa wakiishi kulingana na yale aliyokuwa akisoma katika Biblia. Kwa mfano, watu wengine walipewa chakula kizuri na vipofu walipewa chakula kilichobaki. Mingjie aliumizwa sana na ukosefu huo wa haki, kwa hiyo akaanza kutafuta makanisa mengine katika eneo analoishi. Hiyo ndiyo sababu Mingjie alianza kusali Mungu amsaidie kupata kutaniko la kweli la Kikristo.

Akiwa amependezwa sana na tendo la fadhili la Yanmei, Mingjie alikubali kujifunza Biblia pamoja naye. Baada ya muda, Mingjie alihudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza. Anasema hivi: “Sitasahau kamwe mara yangu ya kwanza kuhudhuria mkutano. Ndugu na dada walinisalimu kwa uchangamfu. Niliguswa moyo sana. Ijapokuwa mimi ni kipofu, nilihisi upendo usio na ubaguzi.”

Mingjie aliendelea kufanya maendeleo na kuanza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Alifurahia hasa kuimba nyimbo za Ufalme, lakini haikuwa rahisi kwake kuimba nyimbo hizo kwa sababu kitabu cha nyimbo hakikupatikana katika maandishi ya vipofu ya Kichina. Kwa hiyo, kwa msaada wa kutaniko lote Mingjie alitengeneza kitabu chake cha nyimbo. Ilimchukua jumla ya saa 22 tu kunakili nyimbo zote 151! Aprili 2018, Mingjie alianza kuhubiri na baada ya muda akaanza kutumia saa 30 kila mwezi kuhubiri.

Kunakili kitabu kwenda kwenye maandishi ya vipofu si kazi rahisi

Ili kumsaidia Mingjie ajiandae kwa ajili ya ubatizo, Yanmei alitengeneza rekodi ya sauti yenye maswali na mistari ya Biblia iliyo katika kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Mungu. Julai 2018, Mingjie alibatizwa. Anasema hivi: “Niliguswa moyo sana na upendo ulioonyeshwa na ndugu na dada katika kusanyiko hilo. Nilitokwa na machozi kwa sababu, hatimaye, nilikuwa sehemu ya kutaniko la kweli la Mungu.” Sasa, Mingjie ameazimia kuonyesha upendo kama ule alionyeshwa, na sasa anatumikia kama mweneza injili wa wakati wote.

a Majina yamebadilishwa