Hamia kwenye habari

Mafuriko Yaliyotokeza Habari Njema

Mafuriko Yaliyotokeza Habari Njema

Mnamo 2017, Mashahidi 12 walifunga safari kwa mashua kutoka eneo la Pwani ya Mosquito (Miskito) nchini Nikaragua. Mashua yao iliitwa Sturi Yamni. Mmoja kati yao anayeitwa Stephen anasema hivi: “Lengo letu lilikuwa kuwatia moyo Mashahidi wachache wanaoishi katika eneo la mbali na kuwasaidia kuhubiri habari njema katika eneo lao pana.”

Mashahidi hao 12 walitoka kwenye Wangwa wa Pearl na kusafiri umbali wa kilomita 200 kwenye mto Río Grande de Matagalpa. Hawakujua kwamba jina la mashua yao, inayomaanisha “Habari Njema” katika lugha ya Miskito, ingekuja kuwa na maana ya pekee kwa watu wanaoishi kando ya mto huo. Baada ya kusafiri kwa saa 12, bila kuhesabu kwamba walilala sehemu fulani usiku, Mashahidi hao walifika mwisho wa safari yao—jamii ya La Cruz de Río Grande. Mashahidi sita wa eneo hilo waliwakaribisha kwa uchangamfu ndugu na dada zao wa kiroho.

Lakini usiku huo hali ikawa mbaya. Dhoruba kubwa ilitokeza mvua kubwa kwenye chanzo cha Río Grande de Matagalpa. Baada ya saa chache tu, mto huo ulivunja kingo zake na maji yake yakaendelea kupanda kwa siku mbili. Maji yalifurika katika Jumba la Ufalme na katika nyumba nyingi katika eneo la La Cruz. Akina ndugu waliokuwa wametembelea eneo hilo waliwasaidia watu wa eneo hilo kuondoka nyumbani. Wengi wao walilala siku mbili katika nyumba ya Shahidi yenye orofa mbili.

Jumba la Ufalme lililofurika la La Cruz

Usiku wa tatu, meya wa La Cruz alienda kuwaona Mashahidi waliokuwa wametembelea eneo hilo ili kuwaomba msaada. Kwa kuwa Sturi Yamni ndiyo mashua pekee iliyokuwa imara kiasi cha kusafiri kwenye mto huo uliofurika, meya alitaka akina ndugu wawasafirishe wafanyakazi wa kutoa msaada ili wakasaidie jamii nyingine zilizoathiriwa. Mashahidi walikuwa tayari kutoa msaada huo.

Siku iliyofuata, Mashahidi watatu waliondoka pamoja na wafanyakazi hao. Stephen anasema hivi: “Kufikia wakati huo mto ulikuwa umefurika. Miti mikubwa ilikuwa ikibebwa na mkondo, maji yalikuwa yakizunguka-zunguka kwa kasi katika maeneo fulani, na maji ya mto yalikuwa yakitiririka kwa mwendo wa zaidi ya kilomita 18 kwa saa.” Licha ya hali hizo ngumu, mashua hiyo iliwafikia watu wa jamii tatu.

Mashahidi hao watatu walitumia nafasi hiyo kuwafariji sana wanakijiji. Pia, Mashahidi walisambaza nakala za toleo la Amkeni! la mwaka 2017 lenye kichwa kinachofaa “Majanga Yanapotokea—Unachoweza Kufanya Ili Uokoke.”

Wakazi wa maeneo hayo yaliyo karibu na mto huo walithamini sana msaada halisi na wa kiroho ambao Mashahidi waliwapa. Baadhi ya wanakijiji walisema, “Mashahidi walikuwa tayari kutusaidia wakati wa taabu.” Wengine walisema, “Wanawapenda jirani zao kikweli.” Baada ya kuona jitihada za Mashahidi hao za kuwasaidia waabudu wenzao na watu wengine, sasa wanakijiji wengi wako tayari kusikiliza ujumbe wa Biblia unaofariji.

Marco, akitoka kwenye mashua ya Sturi Yamni ili kuwahubiria wanakijiji habari njema

Mashua ya Sturi Yamni ikiwa imetia nanga kwenye kijiji kilichokumbwa na mafuriko