Hamia kwenye habari

‘Yehova Aliyaokoa Maisha Yetu’

‘Yehova Aliyaokoa Maisha Yetu’

 Mwaka wa 2005, mwanamke mmoja kutoka India anayeitwa Sowbhagya alifiwa na mume wake mpendwa. Alikuwa akiwatunza vizuri Sowbhagya na binti yao, Meghana, aliyekuwa na umri wa miaka mitatu. Hata hivyo, baada ya mume wake kufa ilikuwa vigumu sana kwa Sowbhagya kupata mahitaji ya lazima.

 Mambo yalizidi kuwa mabaya kwa sababu watu walimdharau na kumbagua Sowbhagya. Watu wa familia yake walimtendea yeye na binti yake kama ombaomba, na waliwaambia tena na tena kwamba walikuwa mzigo kwao. Akitafuta faraja Sowbhagya alianza kuhudhuria ibada katika kanisa la eneo lao lakini watu kanisani humo walimdharau kwa sababu alikuwa maskini. Sowbhagya alianza kutafuta ajira ili aweze kujitegemea. Ingawa alijitahidi sana kutafuta kazi, hakupata.

 Sowbhagya anasema: “Nilikata tamaa na nikaamua kujiua. Hata hivyo, nilijua kwamba ikiwa ningemwacha binti yangu angepata shida nyingi. Basi nikaamua kwamba afadhali tufe sote wawili.” Kwa kuwa Sowbhagya alihisi hafai na hakuna mtu anayempenda, aliamua kwenda kununua sumu.

 Alipokuwa kwenye gari-moshi akirudi nyumbani, Shahidi wa Yehova anayeitwa Elizabeth alianza kuzungumza naye. Sowbhagya alimweleza kwamba hana kazi na kwa fadhili, Elizabeth akamwambia kwamba atamsaidia kutafuta kazi. Elizabeth pia alimwambia kwamba alikuwa akielekea kwenye funzo la Biblia. Sowbhagya alishangaa sana kwa sababu ingawa alikuwa ametembelea makanisa mengi hakuwahi kusikia kuhusu kuwa na funzo la Biblia. Elizabeth alimwalika Sowbhagya amtembelee nyumbani ili ampe maelezo zaidi kuhusu funzo la Biblia.

 Sowbhagya alipofika nyumbani bado alikuwa na mpango wa kujiua. Hata hivyo, mtu wa ukoo alikuwa amesafiri pamoja na Meghana, basi Sowbhagya akaamua kwamba atasubiri hadi binti yake arudi ili atekeleze mpango wake.

 Huku akisubiri, alimtembelea Elizabeth ambaye alimkaribisha kwa uchangamfu. Elizabeth alimwonyesha kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Sowbhagya alipendezwa na sura yenye kichwa “Wafu Wako Wapi?” kwa sababu alikuwa amempoteza mume wake hivi karibuni. Siku hiyohiyo, Sowbhagya alikubali kuanza kujifunza Biblia.

 Elizabeth alimwalika Sowbhagya aje kwenye kusanyiko ambalo lingefanyika baada ya juma moja na alikubali kwenda. Programu hiyo ilimgusa moyo sana hivi kwamba akaamua kuwa Shahidi wa Yehova. Alipokuwa akirudi nyumbani kutoka kusanyikoni alipata kazi ya kuajiriwa.

 Sowbhagya aliendelea kujifunza Biblia. Hakutaka tena kutoa uhai wake kwa sababu alikuwa amepata kusudi maishani. Alibatizwa na baadaye binti yake, Meghana, alibatizwa pia. Leo, wote wawili wanatumikia wakiwa mapainia wa kawaida na Meghana anajitolea kusaidia kazi katika ofisi moja ya utafsiri iliyo India, siku chache kwa juma.

Sowbhagya akiwa na Meghana

 Sowbhagya na Meghana wanafurahi sana kwamba Elizabeth aliongea na Sowbhagya kwenye gari-moshi, akamwonyesha upendo na kumweleza kuhusu kweli! Wanathamini sana jambo ambalo Yehova amewafanyia. Meghana anasema: “Tungekufa zamani ikiwa hatungepata kweli siku hiyo. Sasa, tuna furaha sana. Mimi na mama yangu tunasubiri kwa hamu wakati ambapo tutamkumbatia baba tena na kumweleza kumhusu Yehova na jinsi alivyoyaokoa maisha yetu.”