Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watafsiri Wawili Waliorudisha Jina la Mungu Katika Agano Jipya

Watafsiri Wawili Waliorudisha Jina la Mungu Katika Agano Jipya

 Sala ambayo watu wengi hujifunza kwanza ni Sala ya Bwana, ambayo Yesu aliwafundisha wafuasi wake. Sala hii inapatikana katika sehemu ya Biblia ambayo mara nyingi inaitwa Agano Jipya. Sala hiyo inaanza kwa kusema: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe [au litukuzwe].” (Mathayo 6:9) Hata hivyo, jina la Mungu, ambalo katika Kiswahili huandikwa kuwa “Yehova” au nyakati nyingine “Yahweh,” linapatikana mara chache katika tafsiri za Kiingereza za Agano Jipya. Hata hivyo, tafsiri hizo zinatia ndani majina ya miungu ya uwongo kama vile Zeu, Herme, na Artemi. Kwa hiyo, je, hazipaswi kutaja jina la Mungu wa kweli na Mtungaji wa Biblia?​—Matendo 14:12; 19:35; 2 Timotheo 3:16.

Agano Jipya linataja majina ya miungu kadhaa ya uwongo, je, usingetazamia kwamba litataja jina la Mungu wa kweli vilevile?

 Watafsiri wa Biblia ya Kiingereza Lancelot Shadwell na Frederick Parker waliamini kwamba jina la Mungu lilipaswa kurudishwa katika Agano Jipya. Kwa nini tuseme “kurudishwa”? Kwa sababu walifikia mkataa kwamba hapo awali jina la Mungu lilikuwepo lakini likaondolewa. Kwa nini walifikia mkataa huo?

 Shadwell na Parker walitambua kwamba hati zilizopo za kile kinachoitwa Agano la Kale, ambazo ziliandikwa hasa kwa Kiebrania, zilitia ndani jina la kibinafsi la Mungu mara elfu nyingi. Kwa hiyo, walijiuliza kwa nini hati zilizokuwepo za Agano Jipya hazikuwa na jina kamili la Mungu. a Pia, Shadwell alitambua kwamba hati za Agano Jipya zinapotumia maneno ya kawaida ya Agano la Kale, kama vile “malaika wa Yehova,” wanakili wa Agano Jipya la Kigiriki walikuwa wamebadili jina la Mungu na kutumia maneno kama vile Kyʹri·os, linalomaanisha “Bwana.”​—2 Wafalme 1:3, 15; Matendo 12:23.

Jina la Mungu katika Kiebrania

 Hata kabla ya Shadwell na Parker kuchapisha tafsiri zao za Kiingereza, watafsiri wengine walikuwa wamerudisha jina la Mungu katika tafsiri zao za Kiingereza za Agano Jipya, lakini katika sehemu chache tu. b Kabla ya 1863, Parker alipochapisha A Literal Translation of the New Testament, hakuna mtafsiri wa Kiingereza anayejulikana kuwa alirudisha jina la Mungu katika sehemu nyingi katika Agano Jipya lililochapishwa. Lancelot Shadwell na Frederick Parker walikuwa akina nani?

Lancelot Shadwell

 Lancelot Shadwell (1808-1861) alikuwa wakili na mwana wa Bwana Lancelot Shadwell, naibu wa chansela wa Uingereza. Mwana huyo alikuwa mshiriki wa Kanisa la Uingereza. Ingawa aliamini Utatu, aliheshimu jina la Mungu na kulifafanua kuwa “jina tukufu la YEHOVA.” Katika tafsiri yake, The Gospels of Matthew, and of Mark, alitumia jina “Yehova” mara 28 katika maandiko na mara 465 katika maandishi ya pembeni.

 Huenda Shadwell alijifunza kuhusu jina la Mungu alipoliona katika Agano la Kale na katika Kiebrania cha awali. Alisema kwamba wale ambao walibadili jina la Mungu na kutumia neno Kyʹri·os katika tafsiri ya Kigiriki ya Agano la Kale “hawakuwa watafsiri wanyoofu.”

The Gospel according to Matthew (Injili kulingana na Mathayo), iliyotafsiriwa na L. Shadwell (1859), katika Kiingereza pamoja na maelezo, imeandaliwa na Bodleian Libraries. Leseni ya CC BY-NC-SA 2.0 UK. Sehemu iliyobadilishwa: Maandishi yametiwa alama

Tafsiri ya Shadwell inayoonyesha Mathayo 1:20

 Katika tafsiri yake, Shadwell alituma jina “Yehova” kwa mara ya kwanza kwenye Mathayo 1:20. Maandishi yake kuhusu mstari huo yanasema hivi: “Neno [Kyʹri·os] hapa, na katika mistari mingine mingi ya Agano Jipya linamaanisha YEHOVA, jina linalofaa la Mungu: na ni muhimu sana kurudisha jina hili katika tafsiri ya Kiingereza.” Alisema hivi pia: “Tunapaswa kufanya hivyo ili tumheshimu Mungu. Amejitangaza kwa kutumia jina YEHOVA: na hatuwezi kufanya jambo bora kuliko kulitumia jina hilo tunapozungumza kumhusu.” Kisha akasema: “Katika tafsiri yetu ya Biblia ya E.V. [Established, Authorized, au King James Version], jina YEHOVA linapatikana mara chache sana . . . Badala ya jina linalofaa la Mungu, tunasoma, Bwana.” Shadwell alisema: “Bwana . . . ni jina lisilo na heshima hata kidogo” kutumiwa kama mbadala wa jina la Mungu, na akaongezea kusema kwamba hata yeye anaitwa “Bwana” katika makao yake.

“[Mungu] amejitangaza kwa kutumia jina YEHOVA: na hatuwezi kufanya jambo bora kuliko kulitumia jina hilo tunapozungumza kumhusu.”​—Lancelot Shadwell

 Shadwell alichapisha tafsiri yake ya Mathayo katika mwaka wa 1859 na akachapisha tafsiri yake iliyounganishwa ya Mathayo na Marko katika mwaka wa 1861. Halafu kazi yake ikafikia mwisho. Alikufa Januari 11, 1861, akiwa na umri wa miaka 52. Hata hivyo, jitihada zake hazikuwa za bure.

Frederick Parker

 Mfanyabiashara tajiri aliyeishi London anayeitwa Frederick Parker (1804-1888) alisikia kuhusu tafsiri ya Shadwell ya Mathayo. Parker alikuwa ameanza kutafsiri Agano Jipya alipokuwa na umri wa miaka 20 hivi. Tofauti na Shadwell, Parker hakuamini fundisho la Utatu. Aliandika hivi: “Kanisa lote la Mwana mpendwa [wa Mungu] . . . linapaswa kukubali ukweli kwa moyo wote . . . na kumwabudu Yehova Mweza-Yote mmoja.” Pia, Parker alihisi kwamba hati za Agano Jipya zinazotumia neno Kyʹri·os kumaanisha Bwana Mungu na pia Bwana Yesu, zilificha tofauti iliyopo kati yao wawili. Kwa hiyo, alifurahi kuona kwamba katika muktadha mbalimbali Shadwell alitafsiri Kyʹri·os kuwa “Yehova.”

 Parker alielewaje mambo kama hayo? Alisomea Kigiriki na aliandika vitabu na trakti kadhaa kuhusu sarufi ya Kigiriki. Pia alikuwa mshiriki wa Taasisi ya Uingereza ya Biblia (Anglo-Biblical Institute), ambayo ilichochea utafiti wa hati za Biblia ikiwa na lengo la kutokeza Biblia bora zaidi za Kiingereza. Katika 1842, Parker alianza kuchapisha tafsiri yake ya kwanza ya Agano Jipya katika sehemu na matoleo mbalimbali. c

Tafsiri ya Agano Jipya ya Parker (Heinfetter)

Jitihada za Parker za Kulirudisha Jina la Mungu

 Kwa miaka kadhaa, Parker alikuwa ameandika kuhusu maswali kama vile: “Ni wakati gani ambapo Kyʹri·os inamwakilisha Bwana Yesu, na ni wakati gani inamwakilisha Bwana Mungu?” “Kwa nini neno Kyʹri·os hutumiwa mara nyingi kisarufi kama jina la kibinafsi na si kama jina la cheo?”

 Parker alipoona tafsiri ya Shadwell ya Mathayo mnamo 1859 pamoja na maelezo yake kuhusu Kyʹri·os, alisadiki kwamba katika muktadha mbalimbali, Kyʹri·os “linapaswa kutafsiriwa kuwa Yehova.” Kwa hiyo, alirekebisha tafsiri yake yote ya Agano Jipya ili kutia ndani “Yehova” mahali ambapo aliamini muktadha au sarufi ya maandishi ya Kigiriki ilionyesha jina hilo linapaswa kuwa. Hivyo, katika toleo la Parker la 1863, A Literal Translation of the New Testament, lililotolewa katika buku moja, jina la Mungu linapatikana mara 187 katika maandiko. Inaonekana kwamba hilo ndilo toleo la kwanza la Kiingereza lililochapishwa linalotumia jina la Mungu kotekote katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. d

Ukurasa wenye kichwa wa tafsiri ya Agano Jipya ya 1864 ya Parker

 Mwaka wa 1864, Parker alitoa pia A Collation of an English Version of the New Testament . . . With the Authorized English Version. Sababu yake ya kuunganisha tafsiri hizo mbili za Agano Jipya katika buku moja lilikuwa kuonyesha maeneo na jinsi tafsiri hizo mbili zilivyotofautiana. e

 Ili kuonyesha umuhimu wa kurudisha jina la Mungu, Parker alionyesha mistari kadhaa katika Authorized Version, kutia ndani Waroma 10:13, inayosema: “Kila atakayeliitia jina la Bwana ataokolewa.” Parker aliuliza: “Je, kuna yeyote anayetumia Authorized English Version aliyewahi kuelewa kutokana na Mistari hii kwamba ni Yehova anayerejelewa na si Mwana Yesu Kristo Bwana wetu”?

Waroma 10:13 katika King James Version (juu) na katika tafsiri ya Parker ya 1864

 Parker alitumia maelfu ya pauni, ambazo wakati huo zilikuwa pesa nyingi sana, kuchapisha na kutangaza trakti, majarida, na maandishi yake mengine. Kwa kweli katika mwaka mmoja tu, alitumia pauni 800, zinazolingana na zaidi ya pauni 100,000 (dola 132,000 za Marekani) leo. Pia aliwatumia marafiki na viongozi wa dini wenye wadhifa wa juu nakala za bure za machapisho yake mengi ili wazichunguze.

 Maandishi ya Parker na tafsiri zake za Agano Jipya, ambazo hazikuchapishwa sana, zilidhihakiwa na wasomi kadhaa. Hata hivyo, kwa kufanya hivyo walionyesha kuwa hawakuthamini jitihada za unyoofu ambazo yeye, pamoja na Shadwell na wengine, walifanya ili kulirudisha jina la kibinafsi la Mungu katika Agano Jipya la Kiingereza.

 Huenda ukapenda pia kutazama video ya dakika kumi yenye habari nyingi: Kutembelea Maonyesho ya Warwick: “Biblia na Jina la Mungu.”

a Neno “Yah,” ambalo ni ufupisho wa jina “Yehova,” linapatikana katika Ufunuo 19:1, 3, 4, 6 katika neno “Haleluya,” linalomaanisha “Msifuni Yah, enyi watu!”

b Shadwell hakutafsiri Agano Jipya lote. Watafsiri wale wengine wanatia ndani Philip Doddridge, Edward Harwood, William Newcome, Edgar Taylor, na Gilbert Wakefield.

c Ili kutofautisha shughuli zake za kibiashara na usomi wake wa Biblia, Parker alitumia jina Herman Heinfetter katika maandishi yake ya kidini na katika tafsiri zake za Biblia. Jina hilo linapatikana mara kadhaa katika nyongeza za Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

d Katika 1864, Parker alitoa An English Version of the New Testament inayotumia jina la Mungu mara 186.

e Kabla ya tafsiri za Parker, tafsiri nyingi za Kiebrania za Agano Jipya zilitumia jina la Mungu katika mistari mbalimbali. Pia, katika mwaka wa 1795, Johann Jakob Stolz alichapisha tafsiri ya Kijerumani inayotumia jina la Mungu zaidi ya mara 90 katika Mathayo hadi Yuda.