Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuwasiliana na Vijana Wanaobalehe

Kuwasiliana na Vijana Wanaobalehe

Siri ya Furaha ya Familia

Kuwasiliana na Vijana Wanaobalehe

“Zamani ilikuwa rahisi kuzungumza na mwanangu, lakini kwa kuwa sasa ana umri wa miaka 16, ni vigumu kwangu na kwa mume wangu kujua anachofikiria. Yeye anapendelea kuwa chumbani mwake na hazungumzi nasi mara nyingi!”—MIRIAM, MEXICO.

“Kuna wakati ambapo watoto wangu walitamani sana kunisikiliza. Nao wangenisikiliza kwa makini. Lakini sasa kwa sababu wanabalehe, wanafikiri kwamba siwezi kuwaelewa.”—SCOTT, AUSTRALIA.

IKIWA una kijana anayebalehe, huenda unaelewa kinachosemwa na wazazi walionukuliwa hapo juu. Huenda zamani wewe na mtoto wako mlizungumza kwa uhuru. Sasa inaonekana kwamba mazungumzo yamekoma. “Mwanangu alipokuwa mtoto, alikuwa akiniuliza maswali mengi,” anasema mama mmoja nchini Italia anayeitwa Angela. “Sasa mimi ndiye ninayeanzisha mazungumzo. Nisipofanya hivyo, siku zinaweza kupita bila sisi kuwa na mazungumzo ya maana.”

Kama Angela, pengine umetambua kwamba mtoto wako aliyependa kuzungumza sana, siku hizi amebadilika na kuwa mnyamavu. Huenda ukapata majibu mafupi unapojitahidi kuwasiliana naye. “Habari za leo?” unamwuliza mwana wako. “Nzuri,” anajibu bila uchangamfu. “Mlifanya nini shuleni leo?” unamwuliza binti yako. “Hakuna,” anasema bila kujali. Ukijaribu kuanzisha mazungumzo kwa kuuliza “kwa nini siku hizi huzungumzi?” hupati jibu lolote.

Bila shaka, vijana fulani hawana tatizo la kuzungumza. Hata hivyo, kile wanachosema ni tofauti na kile ambacho wazazi wao walitarajia. “‘Achana na mimi,’ ndivyo alivyonijibu binti yangu nilipomwomba afanye jambo,” anakumbuka mama mmoja nchini Nigeria anayeitwa Edna. Ramón anayeishi Mexico, anakabiliana na hali kama hiyo anaposhughulika na mwanaye mwenye umri wa miaka 16. “Tunabishana karibu kila siku,” anasema. “Kila ninapomwomba afanye jambo, yeye anatoa sababu za kuepuka kulifanya.”

Kujaribu kuwasiliana na kijana asiyetaka kuzungumza kunaweza kuwafanya wazazi wakate tamaa. Biblia inakubali kwamba “mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri.” (Methali 15:22) “Wakati sijui mwanangu anafikiria nini, mimi ninakasirika sana hivi kwamba ninataka kupiga mayowe,” anasema Anna, anayeishi Urusi ambaye ni mzazi asiye na mwenzi. Ni kwa nini katika kipindi ambapo ni muhimu kwa vijana na wazazi kuwasiliana, ndipo wanaposhindwa kuwasiliana?

Kutambua Vikwazo vya Mawasiliano

Mawasiliano yanahusisha mengi zaidi ya kuzungumza. Yesu alisema kwamba ‘kutokana na wingi wa moyo kinywa husema.’ (Luka 6:45) Hivyo basi, kupitia mawasiliano mazuri tunajifunza kutoka kwa wengine na tunafunua mambo yanayotuhusu. Si rahisi kwa vijana kufunua mambo yanayowahusu kwani hata watoto ambao walikuwa wakizungumza sana, wanapoanza kubalehe huenda ghafula wakawa wanyamavu. Wataalamu wanasema kwamba kwa kawaida vijana wanahisi kana kwamba kila kitu wanachofanya na kusema kinachunguzwa na kila mtu. Kwa hiyo, ili kuepuka kuchunguzwa huenda vijana wenye haya wakajitenga, na hivyo kuwazuia wazazi wao kuwafikia.

Kikwazo kingine cha mawasiliano ni tamaa ya kijana ya kujitegemea. Hilo haliwezi kuepukika kwa sababu mtoto wako anakua na hilo linahusisha kujitenga na familia. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba sasa kijana wako yuko tayari kuondoka nyumbani. Bado anakuhitaji katika mambo mengi. Lakini hatua za kutengana zinaanza miaka mingi kabla ya kuwa mtu mzima. Wanapojaribu kufikia ukomavu, vijana wengi wanapendelea kufikiria mambo peke yao kwanza kabla ya kuwaeleza watu wengine mawazo yao.

Ni kweli kwamba mara nyingi vijana wanawaeleza vijana wenzao mambo yao ya kibinafsi, jambo ambalo Jessica, mama kutoka Mexico amejionea. “Alipokuwa mdogo, binti yangu alinijia kila mara alipokuwa na matatizo,” anasema. “Sasa yeye anawaendea marafiki wake.” Ikiwa hali iko hivyo kuhusu kijana wako, usikate kauli kwamba amekukataa kama mzazi. Badala ya hivyo, uchunguzi unaonyesha kwamba hata ikiwa vijana hawakubali, wanathamini mashauri ya wazazi wao kuliko yale ya marafiki wao. Hata hivyo, unaweza kuhakikisha jinsi gani kwamba mawasiliano yanaendelea?

Siri ya Kufaulu Ni Kuondoa Vikwazo

Hebu wazia kwamba unaendesha gari kwenye barabara ndefu iliyonyooka. Kwa kilomita nyingi, umehitaji kugeuza usukani kidogo sana. Kisha, ghafula, kuna kona kali katika barabara. Ili gari lako libaki barabarani, lazima ugeuze usukani. Hali iko vivyo hivyo mtoto wako anapobalehe. Kwa miaka kadhaa, mbinu zako za kuwasiliana naye labda hazijabadilika sana. Lakini sasa, maisha ya mtoto wako yamebadilika sana, na unahitaji ‘kupiga kona’ kwa kubadili mbinu zako za kuwasiliana. Jiulize maswali yafuatayo.

‘Mwana au binti yangu anapokuwa tayari kufunua moyo wake, je, mimi ninakuwa tayari kuwasiliana naye?’ Biblia inasema: “Neno linalosemwa wakati unaofaa ni kama matunda ya mtofaa ya dhahabu kwenye chombo cha fedha kilichopambwa.” (Methali 25:11) Kama andiko hilo linavyoonyesha waziwazi, mara nyingi ni muhimu kuchagua wakati unaofaa. Kwa mfano: Mkulima hawezi kuharakisha au kuchelewesha wakati wa mavuno. Ni lazima avune wakati unaofaa. Huenda kuna wakati hususa ambapo kijana wako anapenda kuzungumza. Tumia nyakati hizo vizuri. “Mara nyingi, binti yangu alikuja chumbani mwangu usiku, na wakati mwingine hata alikaa kwa saa nzima,” anasema Frances, mama asiye na mwenzi anayeishi Australia. “Mimi sipendi kuchelewa kulala, kwa hiyo haikuwa rahisi, lakini katika pindi hizo za usiku, tulizungumza kuhusu kila kitu.”

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Ikiwa kijana wako hapendi kuzungumza, fanyeni jambo fulani pamoja kama vile matembezi, kusafiri kwa gari, kucheza mchezo, au kufanya kazi fulani nyumbani. Mara nyingi, hali kama hizo zinaweza kufanya iwe rahisi kwa kijana kujieleza.

‘Je, ninatambua hisia zinazochochea maneno yake?’ Andiko la Ayubu 12:11 linasema: “Je, sikio halipimi maneno kama kaakaa linavyoonja chakula?” Katika kipindi hiki kuliko wakati mwingine wowote, unahitaji ‘kupima’ kile ambacho mwana au binti yako anasema. Mara nyingi, vijana wanazungumzia mambo kana kwamba yanafanyika hivyo kila wakati. Kwa mfano, mwana au binti yako anaweza kusema, “Sikuzote wewe unanitendea kana kwamba mimi ni mtoto!” au “Hunisikilizi kamwe!” Badala ya kukazia maneno “sikuzote” na “kamwe,” tambua kwamba mtoto wako hayachukulii kwa uhalisi. Kwa mfano, maneno “Sikuzote wewe unanitendea kana kwamba mimi ni mtoto!” yanaweza kumaanisha “Ninahisi kwamba huniamini,” na maneno “Hunisikilizi kamwe!” huenda yakamaanisha “Ninataka kukuambia jinsi ninavyohisi kikweli.” Jaribu kutambua hisia zinazochochea maneno yake.

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Kijana wako anapozungumza kwa hisia, unaweza kusema hivi: “Ninaona kwamba umekasirika, na ninataka kukusikiliza. Nieleze ni kwa nini unahisi kwamba ninakutendea kana kwamba wewe ni mtoto.” Kisha umsikilize bila kumkatiza.

‘Je, bila kujua mimi ninafanya iwe vigumu kuwasiliana na kijana wangu kwa kumlazimisha azungumze?’ Biblia inasema: “Mbegu ya tunda la uadilifu hupandwa chini ya hali zenye amani kwa wale wanaofanya amani.” (Yakobo 3:18) Kupitia maneno na mwenendo wako, fanya kuwe na “hali zenye amani” ili kijana wako ajihisi huru kuzungumza. Kumbuka kwamba wewe ni kama wakili wa kijana wako. Kwa hiyo mnapozungumza kuhusu jambo, usizungumze kana kwamba wewe ni msimamizi wa mashtaka ambaye anajaribu kumkashifu shahidi kortini. “Mzazi mwenye hekima hasemi mambo kama vile ‘Utakomaa lini?’ au, ‘Nimekuambia mara ngapi?’” anasema baba mmoja nchini Korea anayeitwa Ahn. “Baada ya kutoa matamshi kama hayo kwa muda, nilitambua kwamba wana wangu hawakukasirishwa tu na jinsi nilivyozungumza lakini pia na kile nilichosema.”

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Ikiwa kijana wako hataki kujibu maswali, jaribu njia nyingine. Kwa mfano, badala ya kumwuliza binti yako kuhusu siku yake, mweleze jinsi siku yako ilivyokuwa na uone ikiwa atazungumza. Au ili kujua maoni ya mtoto wako kuhusu jambo fulani, mwulize maswali ambayo si ya moja kwa moja. Mwulize jinsi rafiki yake anavyohisi kuhusu jambo hilo. Kisha umwulize anaweza kumpa rafiki yake mashauri gani.

Unaweza kuwasiliana na vijana. Badili mbinu zako za kuwasiliana nao kulingana na uhitaji. Zungumza na wazazi wengine ambao wamefaulu. (Methali 11:14) Unapowasiliana na mwana au binti yako, ‘uwe mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:19) Zaidi ya yote, usife moyo katika jitihada zako za kuwalea vijana wako “katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.”—Waefeso 6:4.

JIULIZE . . .

▪ Nimeona mabadiliko gani tangu mtoto wangu alipoanza kubalehe?

▪ Ninaweza kuboresha uwezo wangu wa kuwasiliana jinsi gani?

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Madokezo Kutoka kwa Wazazi

“Mwanangu huwa anazungumza kwa uhuru tunapokuwa na wengine. Hivyo baadaye, tukiwa peke yetu, mimi ninaendeleza mazungumzo kuhusu mambo tuliyozungumzia mapema.”—ANGELA, ITALIA.

“Tumegundua kwamba watoto wetu wanakuwa tayari kuzungumza nasi ikiwa kwanza tunawapongeza na kuwaambia tunawapenda sana.”—DONIZETE, BRAZILI.

“Nilizungumza na watu wazima waliolelewa kulingana na viwango vya Biblia na nikawauliza jinsi walivyohisi walipokuwa wakibalehe, na jinsi wazazi wao walivyowasaidia. Hilo lilinifundisha mengi.”—DAWN, UINGEREZA.