Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

IGENI IMANI YAO | DAUDI

“Vita Ni vya Yehova”

“Vita Ni vya Yehova”

DAUDI alianza kujitayarisha alipowaona askari wanarudi nyumba. Askari hao walikodoa macho kwa hofu wakiwa katika uwanja wa vita. Ni nini kilichofanya waogope? Lazima iwe Daudi alisikia wakitaja kwa hofu tena na tena kilichofanya waogope. Ni mwanaume fulani. Alikuwa mwenye umbo kubwa na la kutisha, na alikuwa amesimama katika eneo tambarare la bonde, huenda Daudi hakuwahi kumwona mtu kama huyo maishani.

Mtu huyo ni Goliathi! Daudi alipomwona aligundua kwa nini wanajeshi wanamwogopa, Goliathi ni jitu kubwa linaloonekana kutoweza kushindwa. Hata bila silaha zake kubwa, huenda uzito wake ulikuwa zaidi ya watu wazima wawili. Lakini alikuwa mwenye nguvu nyingi, uzoefu mwingi vitani na alijikinga kwa silaha nzito. Goliathi alitoa wito wa ushindani. Wazia sauti yake nzito na kubwa ikisikika katika miteremko ya milima alipokuwa akitukana jeshi la Israeli na mfalme wao Sauli. Anawaambia wachague mtu mmoja ili apigane naye na kumaliza ubishi wa vita hiyo!—1 Samweli 17:4-10.

Waisraeli waliogopa sana. Mfalme Sauli aliogopa pia. Daudi anapata habari kwamba hali hiyo imedumu kwa zaidi ya mwezi mmoja! Majeshi ya Wafilisti na Waisraeli yalibaki kimya Goliathi alipoendelea kudhihaki Waisraeli siku baada ya siku. Hali hiyo ilimhuzunisha sana Daudi. Lilikuwa jambo la kuaibisha kuona mfalme wa Israeli na jeshi lake, kutia ndani kaka zake watatu wameingiwa na woga! Kwa maoni ya Daudi, Goliathi mpagani hatishii tu jeshi la Israeli; bali anafanya jambo baya sana, yaani, kumtukana Mungu wa Israeli, Yehova! Lakini kijana Daudi angefanya nini kuhusu hali hiyo? Tunaweza kujifunza nini kutokana na imani ya Daudi?​—1 Samweli 17:11-14.

“MTIE MAFUTA, KWA MAANA HUYU NDIYE!”

Acheni turudi nyuma miezi mingi mapema. Jioni iliingia Daudi alipokuwa akichunga kondoo za baba yake katika eneo fulani kando ya milima huko Bethlehemu. Huenda bado alikuwa tineja, kijana mwenye sura nzuri, maridadi na makini. Alikuwa na kawaida ya kutumia muda wake kujifunza kupiga kinubi. Uzuri wa uumbaji wa Mungu ulimchochea, na ustadi wake wa muziki uliboreka kwa sababu alitumia muda mwingi kufanya mazoezi aliyofurahia. Lakini jioni moja, Daudi aliitwa nyumbani. Baba yake alihitaji kuzungumza naye.​—1 Samweli 16:12.

Alipofika, alimkuta Yese baba yake akizungumza na mwanaume mzee sana. Alikuwa Samweli, nabii mwaminifu. Yehova alimtuma kumtia mafuta mmoja wa watoto wa Yese, awe mfalme anayefuata wa Israeli! Tayari Samweli alikuwa amewaona kaka saba wa Daudi, hata hivyo, Yehova alimwambia wazi kwamba hakuna aliyemchagua kati yao. Daudi alipofika, Yehova alimwambia hivi Samweli: “Mtie mafuta, maana huyu ndiye!” Samweli akafungua pembe iliyokuwa na mafuta ya pekee, na akayamimina juu ya kichwa cha Daudi mbele ya kaka zake wote. Baada ya kutiwa mafuta, maisha ya Daudi yalibadilika. Biblia inasema hivi: “Na roho ya Yehova ikaanza kutenda kazi juu ya Daudi kuanzia siku hiyo na kuendelea.”​—1 Samweli 16:1, 5-11, 13.

Daudi kwa unyenyekevu alimsifu Yehova kwa kumwezesha kuwaua wanyama mwitu

Je, Daudi alianza kusitawisha tamaa ya kunyakua ufalme? Hapana, aliridhika na kuendelea kusubiri roho ya Yehova imwongoze kujua wakati unaofaa kuanza madaraka hayo mazito. Wakati huohuo, aliendelea kufanya kazi yake ya hali ya chini ya uchungaji, kazi aliyofanya kwa kujidhabihu na ujasiri mwingi. Mara mbili mifugo ya baba yake ilivamiwa, kwanza na simba, kisha na dubu. Daudi hakuwafukuza tu wanyama hao. Badala yake, alipambana ili kulinda kondoo za baba yake. Katika nyakati hizo mbili, aliwaua wanyama hao hatari akiwa peke yake!—1 Samweli 17:34-36; Isaya 31:4.

Baada ya muda Daudi alipata mwaliko. Sifa zake zilimfikia Mfalme Sauli. Ingawa bado alikuwa shujaa mwenye nguvu, Sauli alipoteza kibali cha Yehova kwa kuasi maagizo ya Mungu. Yehova aliondoa roho yake kwa Sauli, hivyo mara nyingi mfalme huyo alitawaliwa na roho mbaya, yaani, hasira, shaka, na jeuri. Roho hiyo mbaya ilipokuwa juu ya Sauli, jambo moja ambalo lingemsaidia kutulia ni muziki. Baadhi ya watu wa Sauli walisikia kuhusu ushujaa wa Daudi na ustadi wake wa muziki. Kwa hiyo Daudi akaitwa, na muda si mrefu akawa mmoja wa wapiga muziki na mchukua silaha wa Sauli.—1 Samweli 15:26-29; 16:14-23.

Vijana wanaweza kujifunza mambo mengi kutokana na imani ya Daudi katika mambo hayo. Ona kwamba Daudi alitumia muda wake kufuatilia miradi iliyomwezesha kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova. Kwa kuongezea, kwa subira alisitawisha stadi mbalimbali zilizofaa na ambazo zilimfanya awe tayari kupata kazi. Zaidi ya yote, alikubali kuongozwa na roho ya Yehova. Bila shaka, hayo ni masomo muhimu ambayo sote tunaweza kujifunza!—Mhubiri 12:1.

“USIACHE MOYO WA MTU YEYOTE UZIMIE NDANI YAKE”

Alipokuwa akimtumikia Sauli, mara nyingi Daudi alirudi nyumbani na kuendelea kuchunga kondoo, nyakati fulani kwa muda mrefu. Katika moja ya vipindi hivyo, Yese alimtuma Daudi kwenda kuwaona kaka zake watatu waliotumikia katika jeshi la Sauli. Daudi alitii na kuchukua mahitaji kwa ajili ya kaka zake, kisha kuelekea Bonde la Ela. Baada ya kufika, alishangazwa kuona majeshi ya Waisraeli na Wafilisti yakiwa tuli bila kupigana kama ilivyoelezwa mwanzoni mwa makala hii. Majeshi hayo yalitazamana kutoka pande mbili za miteremko ya bonde hilo pana.—1 Samweli 17:1-3, 15-19.

Kwa Daudi, hiyo ilikuwa hali isiyoweza kuvumilika. Jeshi la Mungu aliye hai, Yehova, lingewezaje kutishwa na mwanadamu tu, tena mpagani? Daudi aliona dhihaka za Goliathi kuwa ni kumtukana Yehova moja kwa moja. Kwa hiyo akaanza kuzungumza na askari kuhusu kumshinda Goliathi. Baada ya muda mfupi, Eliabu kaka yake, alisikia mazungumzo ya Daudi. Eliabu alimkemea Daudi, na kumlaumu kwa kuja hapo ili tu kushudia mapambano. Lakini Daudi akamjibu hivi: “Sasa nimefanya nini? Je, halikuwa neno tu?” Kisha akaondoka lakini akaendelea kusema kwa ujasiri kuhusu kumshinda Goliathi, mpaka mtu fulani alipomjulisha Sauli maneno ya Daudi. Kisha mfalme akaagiza Daudi aletwe mbele yake.​—1 Samweli 17:23-31.

Daudi alisema maneno haya yenye kutia moyo kwa mfalme kuhusu Goliathi: “Usiache moyo wa mtu yeyote uzimie ndani yake.” Kwa kweli, Sauli na wanaume wake walimwogopa Goliathi. Huenda kwa kufanya kosa la kawaida, yaani, kujilinganisha na jitu hilo, kwa kufikiria kimo chao na kimo chake. Waliwazia kwamba watashindwa kwa urahisi sana. Hata hivyo, Daudi hakufikiri kwa njia hiyo. Kama tutakavyoona, Daudi aliona mambo kwa njia tofauti kabisa. Hivyo, akajitolea kupambana na Goliathi.​—1 Samweli 17:32.

Sauli alipinga kwa kusema hivi: “Wewe huwezi kwenda juu ya huyu Mfilisti kupigana naye, kwa maana wewe ni mvulana tu, naye ni mwanamume wa vita tangu uvulana wake.” Je, ni kweli kwamba Daudi alikuwa mvulana? Hapana, lakini alikuwa na umri mdogo kujiunga na jeshi, na huenda alionekana kijana mdogo. Hata hivyo, tayari Daudi alijulikana kuwa mpiganaji shujaa na huenda alikuwa katika miaka yake ya mwisho ya utineja.​—1 Samweli 16:18; 17:33.

Daudi alimhakikishia Sauli kwa kumsimulia jinsi alivyopambana na simba na dubu. Je, alikuwa akijisifu? Hapana. Daudi alijua kilichomwezesha kushinda mapambano hayo. Alisema hivi: “Yehova, aliyenikomboa kutoka katika makucha ya simba na kutoka katika makucha ya dubu, yeye ndiye atakayenikomboa kutoka mkononi mwa huyu Mfilisti.” Hatimaye Sauli akakubali na kumwambia: “Nenda, na Yehova awe pamoja nawe.”—1 Samweli 17:37.

Je, ungependa kuwa na imani kama ya Daudi? Ona kwamba, imani ya Daudi haikutegemea mambo ya kuwaziwa tu. Alikuwa na imani katika Mungu wake kwa sababu ya ujuzi na mambo aliyojionea. Alijua kwamba Yehova ni Mlinzi mwenye upendo na Mtimizaji wa ahadi zake. Ikiwa tunataka kuwa na imani kama hiyo, tunahitaji kuendelea kujifunza kumhusu Mungu katika Biblia. Tunapoishi kulingana na mambo tunayojifunza, tutapata matokeo mazuri na hilo litaimarisha imani yetu.​—Waebrania 11:1.

“YEHOVA ATAKUTIA MKONONI MWANGU”

Mwanzoni, Sauli alimpa Daudi mavazi yake. Mavazi hayo yalifanana na yale ya Goliathi, yalitengenezwa kwa shaba, na huenda yalitia ndani koti la chuma, lililotengenezwa kwa vipande vya chuma vilivyo kama marinda ya nguo. Daudi alijaribu kutembea akiwa na mavazi hayo makubwa na mazito, hata hivyo, akagundua kwamba hawezi kuyatumia. Hakuwa amezoezwa kuwa askari, hivyo hakuzoea mavazi ya kijeshi, hasa ya Sauli ambaye alikuwa mwanaume mrefu zaidi katika Israeli! (1 Samweli 9:2) Kwa hiyo akatoa mavazi hayo na kuvaa ya kawaida, yaani, yale aliyozoea kuvaa wakati anachunga na kulinda mifugo.​—1 Samweli 17:38-40.

Daudi alichukua fimbo ya kuchungia, mkoba begani mwake, na kombeo. Huenda kombeo ikaonekana kuwa silaha ya kawaida, lakini kwa kweli kombeo ilikuwa silaha hatari. Kombeo ilikuwa na mfuko mdogo katika miisho ya kamba mbili ndefu, na ilikuwa silaha muhimu kwa mchungaji. Mtu aliweka jiwe katika mfuko mdogo, na kuzungusha kwa nguvu juu ya kichwa chake, kisha kuachia kamba moja ili kulenga shabaha. Silaha hiyo ilikuwa bora hivi kwamba nyakati fulani majeshi yalikuwa na kikosi cha watu wenye kombeo.

Akiwa tayari, Daudi aliharakisha ili kukutana na adui yake. Tunaweza kuwazia jinsi Daudi alivyosali kwa bidii aliposimama katika bonde kavu la kijito na kuokota mawe madogo matano, yaliyo laini. Kisha akakimbia ili kwenda kwenye uwanja wa vita!

Goliathi alifikiria nini alipomwona mpinzani wake? Tunasoma hivi: “Akaanza kumdharau kwa sababu alikuwa mvulana tu, mwekundu, na mwenye sura nzuri.” Kisha Goliathi akauliza hivi kwa sauti nzito: “Je, mimi ni mbwa hivi kwamba unijie na fimbo?” Huenda aliiona tu fimbo ya Daudi lakini hakuona kombeo. Kisha alimlaani Daudi kwa majina ya miungu ya Wafilisti na kuapa kuwapatia ndege na wanyama wa porini maiti ya adui yake.​—1 Samweli 17:41-44.

Hadi leo, jibu la Daudi linathibitisha imani yake yenye nguvu. Hebu wazia kijana huyo akimwambia Goliathi hivi: “Unakuja kwangu ukiwa na upanga na mkuki na fumo, lakini mimi naja kwako nikiwa na jina la Yehova wa majeshi, Mungu wa vikosi vya Israeli, ambaye umemtukana.” Daudi alijua kwamba nguvu za mwanadamu na silaha bora si jambo muhimu. Goliathi alimdharau Yehova Mungu na Yehova angechukua hatua. Daudi alisema hivi, “vita ni vya Yehova.”​—1 Samweli 17:45-47.

Haimaanishi kwamba Daudi hakuona kimo na silaha za Goliathi. Hata hivyo, Daudi hakuruhusu mambo hayo yamfanye aogope. Hakufanya kosa ambalo Sauli na wanajeshi wake walifanya. Daudi hakujilinganisha na Goliathi. Badala yake, alimlinganisha Goliathi na Yehova. Ingawa Goliathi alikuwa na urefu wa futi tisa na nusu na kuwazidi watu wengi, kimo hicho kilikuwa bure ukilinganisha na Mwenye enzi kuu ya ulimwengu wote mzima! Kwa kweli, kama ilivyo kwa mtu yeyote, Goliathi alikuwa mdogo zaidi ya mdudu, na katika kisa hiki, mdudu ambaye Yehova alikuwa tayari kumwangamiza!

Daudi alimkimbilia adui yake na kuchukua jiwe katika mkoba wake. Aliliweka katika kombeo na kuizungusha juu ya kichwa chake mpaka ilipokuwa tayari. Goliathi alimkaribia Daudi, huenda akiwa nyuma ya askari aliyembebea ngao. Yaelekea kimo cha Goliathi kilifanya ngao isiwe na faida kwake, kwa kuwa aliyebeba ngao alikuwa na kimo cha kawaida hivyo asingeweza kuinua ngao na kumkinga kichwa. Daudi alitumia fursa hiyo kulenga kichwa.​—1 Samweli 17:41.

Daudi aliona jitu hilo kuwa si kitu ukilinganisha na Yehova Mungu

Daudi alirusha jiwe. Wazia ukimya jiwe lilipoelekea kwa Goliathi. Bila shaka, Yehova alihakikisha kwamba Daudi analenga shabaha. Jiwe likapiga na kuzama moja kwa moja katika paji la kichwa cha Goliathi. Jitu hilo likaanguka chini kifudifudi! Inaelekea mchukua silaha wake alikimbia kwa hofu. Daudi alimkaribia Goliathi na kumkata kichwa kwa upanga wake mwenyewe.​—1 Samweli 17:48-51.

Hatimaye, Sauli na wanajeshi wake wakapata tena ujasiri. Walipiga kelele kubwa za vita na kuwafukuza Wafilisti. Vita ikamalizika kama vile ambavyo Daudi alikuwa amemwambia Goliathi: ‘Yehova . . . atawatia ninyi mikononi mwetu.’​—1 Samweli 17:47, 52, 53.

Leo, watumishi wa Mungu hawashiriki katika vita halisi. Wakati wa kufanya hivyo ulipita. (Mathayo 26:52) Lakini bado tunahitaji kuiga imani ya Daudi. Kama yeye, tunapaswa kumwona Yehova kuwa halisi, yaani, Mungu pekee anayestahili ibada na heshima. Nyakati fulani, huenda tukaona kuwa matatizo tunayokabili ni makubwa sana, hata hivyo, matatizo hayo ni madogo ukilinganisha na Yehova aliye na nguvu zisizo na mipaka. Ikiwa tumemchagua Yehova kuwa Mungu wetu na tumeweka tumaini letu kama Daudi alivyofanya, hakuna changamoto au tatizo linaloweza kutuogopesha. Hakuna jambo linaloweza kuzidi uwezo wa Yehova wa kuokoa!