Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kushirikiana kunamaanisha kuwa kama rubani na msaidizi wake ambao wana lengo lilelile

KWA WENZI WA NDOA

2: Ushirikiano

2: Ushirikiano

MAANA YAKE

Kunapokuwa na ushirikiano katika ndoa, mume na mke wanakuwa kama rubani pamoja na msaidizi wake ambao wana lengo lilelile. Hata changamoto zinapotokea, wao hawasemi “nifanyeje” bali “tufanyeje.”

KANUNI YA BIBLIA: “Wao si wawili tena, bali mwili mmoja.”—Mathayo 19:6.

“Ndoa si suala la mtu mmoja tu. Ni lazima mume na mke washirikiane ili ifanikiwe.” —Christopher.

KWA NINI NI MUHIMU

Matatizo yanapotokea, mume na mke ambao hawana ushirikiano hulaumiana badala ya kufikiria jinsi watakavyotatua tatizo. Matatizo madogo hukuzwa na kuwa kama mlima.

“Ushirikiano ndio msingi wa ndoa. Ikiwa mimi na mume wangu hatushirikiani, tunakuwa tu kama watu wanaoishi chumba kimoja lakini ambao inapohusu kufanya maamuzi muhimu, kila mmoja hutenda kwa njia yake.”—Alexandra.

MAMBO YA KUFANYA

JICHUNGUZE

  • Je, ninaziona pesa ninazopata kuwa ni “zangu tu”?

  • Je, ninahitaji kuwa mbali na mwenzi wangu ili nipate utulivu wa moyo?

  • Je, mimi hujitenga na watu wa ukoo wa mwenzi wangu, hata ingawa yeye ana uhusiano wa karibu na wao?

ZUNGUMZA NA MWENZI WAKO

  • Tunashirikiana zaidi katika nyanja zipi za ndoa yetu?

  • Ni nyanja zipi tunazoweza kuboresha?

  • Tufanye nini ili tuongeze roho ya ushirikiano katika ndoa yetu?

MAPENDEKEZO

  • Jiwazie mkicheza mchezo wa tenisi. Badala ya kumwona mwenzi wako kuwa mpinzani, chukua hatua ili nyote wawili muwe kwenye timu moja mkishambulia matatizo yaliyo upande wa pili.

  • Badala ya kusema, ‘Nifanye nini ili nishinde?’ jiulize ‘Tufanye nini ili tushinde?’

“Usifikirie ni nani aliye sahihi au ni nani mwenye makosa. Hilo si muhimu ukilinganisha na kuwa na amani na umoja katika ndoa yenu.”—Ethan.

KANUNI YA BIBLIA: “Mkiangalia, si faida zenu wenyewe, bali pia faida za wengine.”—Wafilipi 2:3, 4.