Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Marko 1:15​—“Ufalme wa Mungu Umekaribia”

Marko 1:15​—“Ufalme wa Mungu Umekaribia”

 “Wakati uliowekwa umefika, na Ufalme wa Mungu umekaribia. Tubuni na muwe na imani katika habari njema.”—Marko 1:15, Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia. Tubuni na kuiamini Habari Njema!”—Marko 1:15, Biblia Habari Njema.

Maana ya Marko 1:15

 Yesu alisema kwamba Ufalme wa Mungu a ulikuwa “umekaribia” kwa sababu yeye mwenyewe, akiwa Mfalme wa Ufalme huo, alikuwa hapo pamoja nao.

 Yesu hakumaanisha kwamba tayari Ufalme ulikuwa umeanza kutawala. Ukweli ni kwamba, hata baada ya kufufuliwa aliwaonyesha wanafunzi wake kwamba Ufalme ungekuja wakati ujao. (Matendo 1:6, 7) Hata hivyo alikuja duniani kwa wakati unaofaa, katika mwaka uleule ambao Biblia ilitabiri kwamba Mfalme wa wakati ujao angetokea. b Kwa sababu hiyo, Yesu angeweza kusema: “Wakati uliowekwa umefika”​—wakati wa yeye kuanza huduma yake ya hadharani ya kuhubiri injili, au habari njema, inayohusu Ufalme.—Luka 4:16-21, 43.

 Ili kunufaika na habari njema ya Ufalme, watu walihitaji kutubu, yaani, kujutia kutoka moyoni dhambi walizofanya awali na kuishi kulingana na viwango vya Mungu. Wale waliotubu walionyesha kwamba walikuwa na imani katika habari njema kuhusu Ufalme huo wa wakati ujao.

Muktadha wa Marko 1:15

 Yesu alisema maneno haya mwanzoni mwa huduma yake huko Galilaya. Simulizi linalofanana na hilo linalopatikana katika Mathayo 4:17 linaonyesha “Tangu wakati huo,” Yesu alihubiri kuhusu Ufalme wa Mungu. Habari kuu ambayo Yesu alizungumzia wakati wa huduma yake ilikuwa Ufalme. Neno Ufalme linatajwa zaidi ya mara 100 katika vitabu vinne vya Injili c, na mara nyingi ni manukuu ya Yesu mwenyewe. Katika rekodi ya Biblia, Yesu alizungumzia zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu kuliko alivyozungumzia mambo mengine.

Soma Marko sura ya 1 pamoja na maelezo ya chini, marejeo ya pambizoni, picha, na ramani.

a Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni iliyowekwa na Mungu ili kutimiza mapenzi yake duniani. (Danieli 2:44; Mathayo 6:10) Ili kujua mengi zaidi, ona makala yenye kichwa “Ufalme wa Mungu Ni Nini?

b Yesu alipaswa kuwa mfalme ili kutimiza moja ya majukumu yake akiwa Masihi aliyetabiriwa, yaani mwakilishi wa pekee wa Mungu. Kwa habari zaidi ku

husu unabii mbalimbali wa Biblia unaomhusu Yesu akiwa Masihi, ona makala yenye kichwa “Je, Unabii wa Kimasihi Unathibitisha Kwamba Yesu Alikuwa Ndiye Masihi?”

c Injili ni vile vitabu vinne vya kwanza katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, au Agano Jipya, vinavyosimulia maisha ya Yesu na huduma yake.