Hamia kwenye habari

MISTARI YA BIBLIA YAFAFANULIWA

Isaya 40:31—“Wale Wanaomtumaini Yehova Watapata Nguvu Tena”

Isaya 40:31—“Wale Wanaomtumaini Yehova Watapata Nguvu Tena”

 “Lakini wale wanaomtumaini Yehova watapata nguvu tena. Watapaa juu kwa mabawa kama tai. Watakimbia na hawataishiwa na nguvu; watatembea na hawatachoka.”—Isaya 40:31, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

 “Lakini wote wanaomtumainia Mwenyezi-Mungu, watapata nguvu mpya. Watapanda juu kwa mabawa kama tai; watakimbia bila kuchoka; watatembea bila kulegea.”—Isaya 40:31, Biblia Habari Njema.

Maana ya Isaya 40:31

 Yehova a Mungu anawahakikishia waabudu wake kwamba atawapa nguvu wanazohitaji ili kushinda au kuvumilia tatizo lolote wanalokabili.

 “Lakini wale wanaomtumaini Yehova watapata nguvu tena.” Wale ambao wanatumaini, au kuamini, uwezo na utayari wa Mungu wa kuwasaidia watu wake wanaweza kumtegemea awape msaada. (Methali 3:5, 6) Njia moja ambayo Mungu anaweza kuwapa waabudu wake nguvu ni kwa kuwapa roho yake takatifu, au kani ya utendaji.—Luka 11:13.

 “Watapaa juu kwa mabawa kama tai.” Maneno hayo ya mfano yanaonyesha jinsi nguvu za Mungu zinaweza kumwathiri mtu. Tai hutegemea mawimbi ya hewa yenye joto ili aweze kupaa na kunyiririka. Mara tu tai anapopata mawimbi hayo ya hewa yenye joto, anapanua mabawa yake na kuzunguka mawimbi hayo ambayo yanamwinua juu zaidi. Tai anaweza kupaa kwa saa nyingi akihama kutoka wimbi moja hadi lingine, na hivyo kutumia nguvu kidogo sana kufika eneo analoenda.

 “Watakimbia na hawataishiwa na nguvu.” Matatizo maishani yanaweza kutudhoofisha kimwili na kihisia, lakini tunaweza kuvumilia kwa nguvu ambazo Mungu anatupa. Zinaweza kutupatia nguvu za kufanya jambo linalofaa licha ya hali ngumu tunazokabili. Mtume Paulo, ambaye alivumilia majaribu makali, aliandika hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yule anayenipa nguvu.”—Wafilipi 4:13.

Muktadha wa Isaya 40:31

 Mungu alimwongoza kwa roho nabii Isaya aandike maneno hayo katika karne ya nane K.W.K. Ingawa andiko hilo linawahusu watumishi wote waaminifu wa Mungu, huenda Yehova alitumia maneno hayo kuwatia moyo Wayahudi ambao wangepelekwa utekwani Babiloni kwa miaka 70. Wayahudi waliporudi nyumbani kwao baada ya uhamisho huo, waliona maneno ya Mungu yakitimizwa. (Isaya 40:1-3) Mungu aliwapa nguvu za kukamilisha safari hiyo ndefu kwa miguu b kutoka Babiloni hadi Yerusalemu mwaka wa 537 K.W.K.—Isaya 40:29.

a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu.—Zaburi 83:18.

b Njia iliyotumiwa na wahamishwa hao huenda ilikuwa na urefu wa kilomita 1,600 hivi.