Hamia kwenye habari

Sanduku la Agano Ni Nini?

Sanduku la Agano Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Sanduku la agano lilikuwa sanduku takatifu ambalo Waisraeli waliamuriwa na Mungu watengeneze kupatana na maagizo aliyowapa. Sanduku hilo lilikuwa na “ule Ushuhuda,” yaani, zile Amri Kumi zilizoandikwa kwenye mabamba mawili ya mawe.​—Kutoka 25:​8-​10, 16; 31:18.

  •   Ujenzi. Sanduku hilo lilikuwa na urefu wa mikono 2.5, upana wa mkono 1.5, na kimo cha mkono 1.5 (sentimita 111 x 67 x 67). Lilijengwa kwa kutumia mbao za mshita. Nje na ndani mbao hizo zilifunikwa kwa dhahabu, na zilikuwa na ukingo wa kisanii. Kifuniko chake kilitengenezwa kwa dhahabu safi, na kilikuwa na makerubi wawili kwenye kila kona. Nyuso za makerubi hao zilikuwa zikielekeana na mabawa yao yalikuwa yamenyooshwa kuelekea juu, yakifunika kifuniko hicho. Sanduku la agano lilikuwa na pete nne za dhahabu juu ya miguu yake minne. Miti ya mshita iliyofunikwa kwa dhahabu ilitiwa kwenye pete hizo ili kulibeba Sanduku.​—Kutoka 25:10-21; 37:6-9.

  •   Mahali. Sanduku liliwekwa kwenye Patakatifu Zaidi pa maskani. Maskani ilikuwa hema inayoweza kusafirishwa na ilitengenezwa wakati uleule na sanduku la agano. Kulikuwa na pazia lililositiri Patakatifu Zaidi ili pasionekane na makuhani na watu. (Kutoka 40:3, 21) Ni kuhani mkuu peke yake aliyeingia kwenye chumba hicho, siku moja kwa mwaka kwenye Siku ya Upatanisho, na kuliona Sanduku hilo. (Mambo ya Walawi 16:2; Waebrania 9:7) Baadaye, Sanduku lilihamishwa kwenye Patakatifu Zaidi katika hekalu la Sulemani.​—1 Wafalme 6:​14, 19.

  •   Kusudi. Sanduku la agano lilikuwa hifadhi ya vitu vitakatifu ambavyo vingewakumbusha Waisraeli kuhusu agano lao, au makubaliano ambayo Mungu alikuwa amefanya nao kwenye Mlima Sinai. Lilitimiza fungu muhimu kwenye Siku ya Upatanisho.​—Mambo ya Walawi 16:​3, 13-17.

  •   Vilivyomo. Kitu cha kwanza kuingizwa kwenye sanduku la agano kilikuwa yale mabamba ya mawe yaliyokuwa na zile Amri Kumi. (Kutoka 40:20) Baadaye mtungi wa dhahabu uliokuwa na mana pamoja na “ile fimbo ya Haruni iliyochipuka” vilitiwa ndani. (Waebrania 9:4; Kutoka 16:33, 34; Hesabu 17:10) Ni wazi kwamba mtungi na fimbo viliondolewa kwa kuwa havikuwa ndani ya Sanduku lilipoingizwa kwenye hekalu.​—1 Wafalme 8:9.

  •   Usafirishaji. Sanduku lilibebwa na Walawi juu ya mabega yao kwa kutumia miti ya mshita. (Hesabu 7:9; 1 Mambo ya Nyakati 15:15) Miti hiyo haikuondolewa kwenye Sanduku hilo, kwa hiyo Walawi hawakuhitaji kugusa sanduku la agano. (Kutoka 25:12-16) “Pazia lenye kusitiri” lililotenganisha Patakatifu na Patakatifu Zaidi lilitumiwa kufunika sanduku la agano lilipokuwa likibebwa.​—Hesabu 4:​5, 6. a

  •   Uwakilisho. Sanduku la agano lilihusianishwa na kuwapo kwa Mungu. Kwa mfano, wingu lililojitokeza juu ya sanduku la agano katika Patakatifu Zaidi na mahali ambapo Waisraeli walipiga kambi lilikuwa ishara ya kuwepo kwa Yehova na baraka zake. (Mambo ya Walawi 16:2; Hesabu 10:33-​36) Pia, ikizungumza kuhusu wale makerubi wanaoketi juu ya sanduku la agano, Biblia inasema kwamba Yehova ‘anaketi juu ya makerubi.’ (1 Samweli 4:4; Zaburi 80:1) Kwa hiyo, makerubi hao walikuwa “mfano wa gari” la Yehova. (1 Mambo ya Nyakati 28:18) Kwa sababu ya kile ambacho Sanduku liliwakilisha, Mfalme Daudi aliandika kwamba Yehova ‘anakaa Sayuni’ baada ya Sanduku hilo kufikishwa huko.​—Zaburi 9:11.

  •   Majina. Biblia inatumia majina kadhaa inaporejelea sanduku hilo takatifu, kutia ndani “sanduku la ushuhuda,” “sanduku la agano,” “sanduku la Yehova,” na “Sanduku la nguvu [za Yehova].”​—Hesabu 7:89; Yoshua 3:6, 13; 2 Mambo ya Nyakati 6:41.

     Kifuniko cha sanduku la agano liliitwa “kifuniko cha upatanisho,” au “kiti cha rehema.” (1 Mambo ya Nyakati 28:11; Union Version) Jina hilo linaonyesha kusudi la pekee la kifuniko wakati wa Siku ya Upatanisho, wakati ambapo kuhani mkuu wa Israeli akiwa mbele ya kifuniko hicho alitapanya damu ya wanyama waliotolewa dhabihu. Kwa kufanya hivyo, kuhani mkuu alifanya upatanisho, au alifunika dhambi “kwa ajili yake mwenyewe na kwa ajili ya nyumba yake na kwa ajili ya kutaniko lote la wana wa Israeli.”​—Mambo ya Walawi 16:14-​17.

Je, sanduku la agano bado lipo hadi leo?

 Hakuna uthibitisho kwamba lipo. Biblia inaonyesha kwamba Sanduku hilo halihitajiki tena kwa kuwa agano linalohusiana na hilo lilibadilishwa na “agano jipya,” linalotegemea dhabihu ya Yesu. (Yeremia 31:31-33; Waebrania 8:13; 12:24) Hivyo, Biblia ilitabiri wakati ambapo sanduku la agano halingekuwepo, lakini watu wa Mungu hawangelihitaji.​—Yeremia 3:​16.

 Katika maono ambayo mtume Yohana alipewa baada ya agano jipya kuanzishwa, sanduku la agano lilionekana mbinguni. (Ufunuo 11:15, 19) Sanduku hilo la agano liliwakilisha kuwapo kwa Mungu na baraka yake juu ya agano jipya.

Je, sanduku la agano lilikuwa na nguvu za pekee?

 Hapana. Kuwa tu na sanduku la agano hakukumaanisha kwamba watu wangepata ufanisi. Kwa mfano, Waisraeli walikuwa na sanduku la agano kambini walipokuwa wanapigana na jiji la Ai, lakini walishindwa kwa sababu ya ukosefu wa uaminifu wa Waisraeli. (Yoshua 7:​1-6) Baadaye, walishindwa na Wafilisti licha ya kwamba walienda na sanduku la agano kwenye uwanja wa vita. Walishindwa kwa sababu ya uovu wa makuhani Waisraeli Hofni na Finehasi. (1 Samweli 2:​12; 4:​1-​11) Wafilisti waliteka sanduku la agano wakati wa vita hivyo, lakini walipatwa na mapigo kutoka kwa Mungu hadi walipolirudisha Israeli.​—1 Samweli 5:11–6:​5.

Historia ya sanduku la agano

Mwaka (K.W.K.)

Tukio

1513

Lilitengenezwa na Bezaleli na wasaidizi wake kwa kutumia vifaa vilivyotolewa na Waisraeli.​—Kutoka 25:​1, 2; 37:1.

1512

Liliwekwa wakfu na Musa pamoja na maskani na ukuhani.​—Kutoka 40:​1-3, 9, 20, 21.

1512​—Baada ya 1070

Linahamishwa maeneo mbalimbali.​—Yoshua 18:1; Waamuzi 20:26, 27; 1 Samweli 1:​24; 3:3; 6:​11-​14; 7:​1, 2.

Baada ya 1070

Linaletwa kutoka Yerusalemu na Mfalme Daudi.​—2 Samweli 6:​12.

1026

Linaingizwa kwenye hekalu ya Sulemani huko Yerusalemu.​—1 Wafalme 8:​1, 6.

642

Linarudishwa hekaluni na Mfalme Yosia.​—2 Mambo ya Nyakati 35:3. b

Kabla ya 607

Inaonekana liliondolewa hekaluni. Halitajwi kati ya vyombo vilivyopelekwa Babiloni hekalu lilipohabiriwa mwaka wa 607 K.W.K. wala halitajwi kati ya vyombo vilivyorudishwa Yerusalemu baadaye.​—2 Wafalme 25:13-​17; Ezra 1:​7-​11.

63

Jenerali Mroma Pompey alisema kuwa linakosekana aliposhinda jiji la Yerusalemu na kukagua Patakatifu Zaidi pa hekalu. c

a Waisraeli walikabili hali mbaya walipoasi sheria ya Mungu kuhusu jinsi ya kusafirisha na kufunika sanduku la agano.​—1 Samweli 6:​19; 2 Samweli 6:​2-7.

b Biblia haisemi liliondolewa lini, kwa nini, au na nani.

c Ona kitabu The Histories, kilichoandikwa na Tacitus, Buku la V, fungu la 9.