Hamia kwenye habari

Neno la Mungu—Ni Nani au Ni Nini?

Neno la Mungu—Ni Nani au Ni Nini?

Jibu la Biblia

 Kwa kawaida, maneno “neno la Mungu” yanawakilisha ujumbe kutoka kwa Mungu au mkusanyo wa ujumbe huo. (Luka 11:28) Katika sehemu chache, “Neno la Mungu” au “Neno” hutumiwa kuwakilisha cheo cha mtu.​—Ufunuo 19:13; Yohana 1:​14.

 Ujumbe kutoka kwa Mungu. Mara nyingi manabii walisema kwamba ujumbe ambao walitoa ulikuwa Neno la Mungu. Kwa mfano, Yeremia alianza ujumbe wake wa kinabii kwa kusema “neno la Yehova likaanza kunijia.” (Yeremia 1:4, 11, 13; 2:1) Kabla ya kumwambia Sauli kwamba Mungu alikuwa amemchagua kuwa mfalme, nabii Samweli alisema hivi: “Simama tuli sasa ili nikuambie neno la Mungu.”​—1 Samweli 9:27.

 Cheo cha mtu. Pia “Neno” linaonekana katika Biblia likiwa cheo cha Yesu Kristo, akiwa roho mbinguni na pia akiwa mwanadamu duniani. Fikiria sababu kadhaa za kufikia mkataa huo:

  •   Neno aliishi kabla ya vitu vingine vyote kuumbwa. “Hapo mwanzo Neno alikuwako . . . Hapo mwanzo huyo alikuwa pamoja na Mungu.” (Yohana 1:1, 2) Yesu ndiye “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote . . . yeye ni wa kabla ya vitu vingine vyote.”​—Wakolosai 1:13-15, 17.

  •   Neno alikuja duniani akiwa mwanadamu. “Neno akawa mwili, akakaa katikati yetu.” (Yohana 1:14) Kristo Yesu “alijiondolea mwenyewe hali yake na kuchukua umbo la mtumwa na kuwa kama wanadamu.”​—Wafilipi 2:5-7.

  •   Neno ni Mwana wa Mungu. Baada ya kusema kwamba “Neno akawa mwili,” kama ilivyonukuliwa hapo juu, mtume Yohana aliendelea kusema hivi: “Nasi tukautazama utukufu wake, utukufu kama ule ulio wa mwana mzaliwa-pekee kutoka kwa baba.” (Yohana 1:14) Pia, Yohana aliandika hivi: “Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu.”​—1 Yohana 4:15.

  •   Neno ana sifa kama za Mungu. “Neno alikuwa mungu.” (Yohana 1:1) Yesu “ndiye mng’ao wa utukufu [wa Mungu] na mwakilisho sawasawa wa utu wake wenyewe.”​—Waebrania 1:2, 3.

  •   Neno anatawala akiwa mfalme. Biblia inasema kwamba kwenye kichwa cha Neno la Mungu “kuna vilemba vingi.” (Ufunuo 19:12, 13) Neno anaitwa pia “Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana.” (Ufunuo 19:16) Yesu anaitwa “Mfalme wa wale wanaotawala wakiwa wafalme na Bwana wa wale wanaotawala wakiwa mabwana.”​—1 Timotheo 6:14, 15.

  •   Neno ni msemaji wa Mungu. Inaonekana kwamba jina la cheo “Neno” linamtambulisha yule ambaye Mungu humtumia kuwasilisha habari na maagizo. Yesu alisema kwamba alitimiza jukumu hilo: “Baba mwenyewe aliyenituma amenipa amri kuhusu jambo la kutangaza na la kusema. . . . Kwa hiyo mambo ninayosema, kama vile Baba alivyoniambia, ndivyo ninavyoyasema.”​—Yohana 12:49, 50.