Hamia kwenye habari

IGENI IMANI YAO | AYUBU

Yehova Alimponya Maumivu Yake

Yehova Alimponya Maumivu Yake

Hatimaye, hao watu wachache wakanyamaza. Huenda sauti pekee iliyokuwa ikisikika ilikuwa ni sauti ya upepo mwanana katika jangwa la Uarabuni. Ayubu aliishiwa na maneno ya kusema, naye alikuwa amechoka baada ya mjadala mrefu. Hebu wazia Ayubu akiwatazama rafiki zake Elifazi, Bildadi, na Sofari—akiwa amechoka kuwasikiliza. Nao hawakuweza kumtazama usoni, mbinu zao za kijanja hazikufanikiwa, maneno yao “ya ubatili”, na mashtaka yao yenye kuumiza hayakufanikiwa. (Ayubu 16:3, maelezo ya chini) Ayubu alikuwa ameazimia kutetea utimilifu wake kwa njia yoyote ile.

Huenda Ayubu alihisi kama utimilifu wake ndio mali pekee aliyokuwa amebaki nayo. Alikuwa amepoteza mali zake zote, watoto wake kumi, urafiki na heshima kutoka kwa jirani zake, na si hayo tu, afya yake ilizorota. Ngozi yake ilikuwa nyeusi kwa sababu ya ugonjwa aliopata, yenye magamba ya vigaga, na mabuu wanaotembea juu yake. Hata harufu iliyotoka kinywani mwake ilikuwa yenye kuchukiza. (Ayubu 7:5; 19:17; 30:30) Na bado, maneno makali ya wale wanaume watatu yalimvuruga Ayubu na kuchochea ghadhabu kali ndani yake. Alipambana kuwahakikishia kwamba yeye si mtenda dhambi kama walivyodhania. Maneno ambayo Ayubu alizungumza mwishoni yaliwanyamazisha kabisa. Hatimaye waliishiwa na maneno. Hata hivyo, bado Ayubu alikuwa na maumivu. Bado alihitaji msaada!

Inaeleweka kwamba njia ya Ayubu ya kufikiri ilikuwa imeathiriwa. Alihitaji kupata mwongozo sahihi na kurekebishwa. Na pia, alihitaji faraja na kuimarishwa, mambo ambayo wale rafiki zake watatu walipaswa kufanya lakini walishindwa. Je, umewahi kuhisi unahitaji mwongozo na kufarijiwa? Je, umewahi kuvunjwa moyo na watu uliodhani ni rafiki zako? Kujifunza jinsi Yehova Mungu alivyomsaidia Ayubu na jinsi Ayubu alivyoitikia kunaweza kukutia moyo na kukupa msaada.

Mshauri Mwenye Hekima na Fadhili

Simulizi la Ayubu linafunua jambo lingine la pekee. Kulikuwa na mtu mwingine karibu nao, mwanamume mwenye umri mdogo aliyeitwa Elihu. Alikuwa kimya akiwasikiliza wanaume hao wenye umri mkubwa wakibishana muda wote huo. Na hakufurahishwa kabisa na mambo aliyosikia wakisema.

Elihu alimkasirikia Ayubu. Aliumia sana kumwona Ayubu, mwanamume mwadilifu akiruhusu kukasirishwa na wanaume hao na kujaribu “kujithibitisha mwenyewe kuwa mwadilifu badala ya Mungu.” Kwa kweli, Elihu alimhurumia sana Ayubu, aliona jinsi anavyoteseka, unyoofu wake na jinsi alivyohitaji kufarijiwa na kushauriwa. Ndiyo sababu Elihu alishindwa kuwavumilia wale wafariji wake watatu wa uwongo! Aliwasikiliza wakimkaripia Ayubu, wakitilia shaka imani yake, heshima yake, na utimilifu wake. Na jambo baya zaidi ni kwamba maneno yao yaliyopotoka yalikuwa yakimtangaza Mungu kuwa mwovu. Inaeleweka kwa nini Elihu alitamani sana kuwakatiza ili azungumze!—Ayubu 32:2-4, 18.

Alisema: “Mimi ni kijana, lakini ninyi ni wazee. Kwa hiyo kwa heshima nilijizuia, nami sikuthubutu kuwaambia ninayojua.” Lakini hakuweza kunyamaza tena. Akaendelea kusema: “Umri peke yake haumfanyi mtu awe na hekima, wala si wazee peke yao wanaoelewa yaliyo sawa.” (Ayubu:6, 9) Hivyo, Elihu alijieleza kwa kina, na kuthibitisha ukweli wa maneno hayo. Alitumia njia tofauti sana na ile ya Elifazi, Bildadi, na Sofari. Elihu alimhakikishia Ayubu kwamba hangemdhihaki au kumwongezea mkazo. Hata alimheshimu Ayubu, akamwita kwa jina na kuonyesha kwamba rafiki zake walikuwa wakimdhihaki. * Kwa heshima alisema: “Lakini sasa, Ayubu, tafadhali sikiliza maneno yangu.”—Ayubu 33:1, 7; 34:7.

Elihu alimtaja Ayubu jina alipozungumza naye na kumtendea kwa fadhili na heshima

Elihu alimpatia Ayubu ushauri ulio wazi akisema: “Lakini nilisikia ukisema, . . . ‘Mimi ni safi, sina dhambi; Mimi ni safi, sina kosa. Lakini Mungu anatafuta sababu za kunipinga.’” Elihu alienda moja kwa moja kwenye chanzo cha tatizo, akauliza: “Je, unasadiki kabisa kwamba uko sahihi hivi kwamba unasema, ‘Mimi ni mwadilifu kuliko Mungu’?” Hangekubaliana na njia hiyo ya kufikiri. Kijana huyo akasema, “Umekosea kusema hivyo.” (Ayubu 33:8-12; 35:2) Elihu alijua kwamba Ayubu alikuwa amejaa ghadhabu kwa sababu alipitia matatizo mengi na hata rafiki zake wa uwongo wakamtendea vibaya. Lakini Elihu alimwonya Ayubu: “Jihadhari ghadhabu isikufanye uwe na chuki.”—Ayubu 36:18.

Elihu Anakazia Fadhili za Yehova

Zaidi ya yote, Elihu alimtetea Yehova Mungu. Kwa kutumia maneno haya alieleza kwa ufupi ukweli huu: “Mungu wa kweli hawezi kamwe kuwazia kutenda uovu, na Mweza-Yote hawezi kamwe kutenda kosa! . . . Mweza-Yote hapotoshi hukumu.” (Ayubu 34:10, 12) Elihu aliiga fadhili za Yehova, kwa kumkumbusha Ayubu kwamba Yehova hakuingilia kati na kumwadhibu Ayubu kwa sababu ya kusema maneno haraka-haraka na bila kufikiri. (Ayubu 35:13-15) Kwa unyenyekevu Elihu alisema: “Mungu ameinuliwa sana kuliko tunavyoweza kujua” na hakudai kwamba anajua kila kitu.—Ayubu 36:26.

Licha ya kwamba ushauri wake ulikuwa wazi, Elihu aliendelea kumwonyesha Ayubu fadhili. Alizungumzia tumaini zuri la wakati ujao, la kwamba siku moja Yehova atamrudishia afya yake njema. Wakati huo Mungu atasema hivi kuhusu mtumishi wake mwaminifu: “Mwili wake na uwe na afya zaidi kuliko wakati wa ujana.” Pia, badala ya kuzungumza kwa mfululizo, Elihu alimwonyesha Ayubu fadhili alipomruhusu azungumze. Alisema hivi: “Sema, kwa maana nataka kuthibitisha kwamba uko sahihi.” (Ayubu 33:25, 32) Lakini Ayubu hakujibu lolote. Huenda hakuhisi kwamba alihitaji kujitetea dhidi ya ushauri uliomtia moyo na uliotolewa kwa fadhili. Labda alilia kwa faraja aliyopata.

Tunaweza kujifunza mambo mengi kutoka kwa wanaume hawa waaminifu. Mfano wa Elihu unatufundisha jinsi tunavyoweza kuwashauri na kuwafariji wale walio na uhitaji. Rafiki wa kweli hatasita kutuambia ikiwa tunafanya makosa makubwa au ikiwa tunafuata mwelekeo usiofaa. (Methali 27:6) Tunapenda kuwa rafiki wa aina hiyo ambaye ataendelea kuwa na fadhili, mwenye kutia moyo, hata ikiwa mtu aliyevunjika moyo anazungumza bila kufikiri. Na ikiwa sisi wenyewe tutahitaji ushauri wa aina hiyo mfano wa Ayubu unatukumbusha kwamba tunapaswa kusikiliza kwa unyenyekevu. Sisi sote tunahitaji ushauri na marekebisho. Tukiukubali tutaokoa maisha yetu.—Methali 4:13.

“Kutoka Katika Dhoruba ya Upepo”

Elihu alipokuwa akizungumza, alitaja mara nyingi maneno upepo, mawingu, mngurumo, na radi. Alisema hivi kumhusu Yehova: “Sikiliza kwa makini mrindimo wa sauti yake.” Baadaye, Elihu alitaja “upepo wa dhoruba.” (Ayubu 37:2, 9) Inaonekana alipokuwa akizungumza, dhoruba ilikuwa ikitokea, na ilizidi kuongezeka hatua kwa hatua. Mwishowe, ikawa dhoruba kali ya upepo. Kisha jambo la kushangaza zaidi likatokea. Yehova akazungumza!—Ayubu 38:1.

Wazia ukisikiliza hotuba kuhusu uumbaji ikitolewa na Muumba mwenyewe wa ulimwengu!

Unaposoma kitabu cha Ayubu, inafariji sana kusoma sura hizi zenye kustaajabisha zilizo na maneno ambayo Yehova alimwambia Ayubu. Ni kana kwamba dhoruba ya upepo wa kweli ilikuwa ikipulizia mbali maneno matupu na uwongo wa Elifazi, Bildadi, na Sofari. Mwanzoni Yehova hakuzungumza na wanaume hao. Alimkazia fikira Ayubu peke yake; alizungumza na mtumishi wake mpendwa kwa uthabiti kama baba anavyomrekebisha mwanaye.

Yehova alielewa uchungu wa Ayubu. Na alimsikitikia Ayubu, kama anavyofanya sikuzote watumishi wake wapendwa wanapoteseka. (Isaya 63:9; Zekaria 2:8) Lakini alijua pia kwamba Ayubu alikuwa “[aki]zungumza bila ujuzi,” na kufanya hali yake iwe mbaya zaidi. Basi Yehova alimrekebisha Ayubu kwa kumuuliza maswali ya kina. Alianza kwa kumuuliza, “Ulikuwa wapi nilipoweka misingi ya dunia? Niambie, ikiwa unafikiri unaelewa.” Mwanzoni mwa uumbaji, “nyota za asubuhi,” familia ya Mungu ya malaika, walishangilia kwa sauti kwa sababu ya maajabu ya uumbaji. (Ayubu 38:2, 4, 7) Ayubu hakuwa na jibu.

Yehova alizungumza kutoka katika dhoruba ya upepo, akirekebisha maoni ya Ayubu kwa upendo

Yehova aliendelea kuzungumza kuhusu kazi zake za uumbaji. Ni kana kwamba alikuwa anamwonyesha kile ambacho watu leo huita sayansi ya asili, akizungumzia mambo kama elimu ya nyota, miamba, biolojia na fizikia. Yehova alizungumzia hasa wanyama ambao walikuwepo siku za Ayubu—simba, kunguru, mbuzi wa milimani, punda mwitu, fahali mwitu, mbuni, farasi, kipanga, tai, Behemothi (inaonekana ni kiboko), na mwishowe Lewiathani (huenda ni mamba). Wazia ukisikiliza hotuba kuhusu uumbaji ikitolewa na Muumba mwenyewe wa ulimwengu! *

Kufundisha Kuhusu Unyenyekevu na Upendo

Lengo la hayo yote lilikuwa nini? Ayubu alihitaji kusitawisha haraka sifa ya unyenyekevu. Kwa kulalamika kuhusu jambo alilodhani kwamba ni kutendewa vibaya na Yehova, Ayubu alikuwa akiongeza maumivu yake, na kujitenga na Baba yake mpendwa. Basi Yehova akamuuliza Ayubu tena na tena alikuwa wapi wakati maajabu hayo yalipotokea na ikiwa Ayubu anaweza kulisha, kudhibiti, au kuwafuga wanyama ambao Yehova aliwaumba. Ikiwa Ayubu hangeweza kudhibiti hata mambo ya msingi ya uumbaji wa Yehova, angewezaje kumhukumu Muumba? Je, si kweli kwamba njia na mawazo ya Yehova yako juu sana kuliko maoni ya Ayubu?

Ayubu hakubishana na Yehova, wala hakujitetea, au kutoa visingizio

Mambo yote ambayo Yehova alisema yaliongozwa na upendo. Ni kana kwamba Yehova alikuwa akimwambia Ayubu: ‘Mwanangu, ikiwa ninaweza kuumba na kutunza viumbe wote hawa, kweli unadhani nitashindwa kukutunza wewe? Je, kweli ninaweza kukuacha, kukunyang’anya watoto, usalama wako, na afya yako? Am Mimi tu ndiye ninayeweza kukurudishia vitu ulivyopoteza na kukuponya kutokana na maumivu yako, sivyo?’

Ayubu alijibu mara mbili tu maswali yenye kuchochea hisia ya Yehova. Hakubishana, hakujitetea, au kutoa visingizio. Kwa unyenyekevu, alikubali kwamba hakujua mengi, na akatubu kwa kuzungumza bila kufikiri. (Ayubu 40:4, 5; 42:1-6) Hapa tunaona vizuri kabisa imani ya Ayubu. Licha ya mambo yote aliyopitia, aliendelea kuwa na imani kubwa. Alikubali marekebisho ya Yehova na kuyaweka moyoni. Sisi pia tunaweza kujiuliza swali hili linalochochea hisia, ‘Am Je, mimi ni mnyenyekevu vya kutosha kukubali marekebisho na ushauri?’ Sote tunahitaji msaada huo. Tunapoukubali, tunaiga imani ya Ayubu.

“Hamkusema Ukweli Kunihusu”

Kisha Yehova akachukua hatua ya kumfariji Ayubu. Akizungumza na Elifazi, ambaye huenda ndiye aliyekuwa na umri mkubwa kati ya wale wafariji watatu wa uwongo, Yehova alisema: “Hasira yangu inawaka dhidi yako na rafiki zako wawili, kwa sababu hamkusema ukweli kunihusu kama alivyofanya mtumishi wangu Ayubu.” (Ayubu 42:7) Fikiria maneno hayo. Je, Yehova alimaanisha kwamba mambo yote ambayo wanaume hao walisema yalikuwa ya uwongo au kwamba kila jambo ambalo Ayubu alisema lilikuwa sahihi? Sivyo hata kidogo. * Hata hivyo, kulikuwa na tofauti kubwa kati ya Ayubu na wanaume hao. Ayubu alikuwa amevunjika moyo, alikuwa amejawa na huzuni, na kulemewa na mashtaka ya uwongo. Basi, inaeleweka kwamba wakati mwingine aliongea bila kufikiri. Hata hivyo, Elifazi na wenzake wawili hawakulemewa na hisia hizo. Kwa sababu ya imani yao dhaifu, walizungumza kimakusudi na kwa kiburi. Walimshambulia mwanamume asiye na hatia, na pia, wakamfanya Yehova aonekane kuwa Mungu mkatili na mwovu!

Haishangazi kwamba Yehova alifanya wanaume hao wawajibike. Walipaswa kutoa dhabihu ya fahali saba na kondoo-dume saba—gharama kubwa, kwa sababu baadaye katika Sheria ya Musa, kuhani angetoa dhabihu ya fahali ikiwa dhambi yake ilileta hatia juu ya taifa lote. (Mambo ya Walawi 4:3) Hiyo ndiyo dhabihu iliyokuwa na gharama ya juu zaidi kati ya dhabihu zilizotajwa katika Sheria. Isitoshe, Yehova alisema kwamba angekubali dhabihu ya wanaume hao ikiwa Ayubu angesali kwanza kwa niaba yao. * (Ayubu 42:8) Ayubu alifarijika sana kutetewa na Mungu na kuona haki ya Yehova ikishinda!

”Mtumishi wangu Ayubu atasali kwa ajili yenu.”—Ayubu 42:8

Yehova alikuwa na hakika kwamba Ayubu angefanya kama alivyaogizwa, angewasamehe wanaume hao waliokuwa wamemuumiza sana. Ayubu alitenda kulingana na maagizo ya Baba yake. (Ayubu 42:9) Utii wake ulikuwa uthibitisho mkubwa zaidi wa utimilifu wake, uthibitisho wenye nguvu kuliko maneno peke yake. Na ulimfungulia Ayubu njia ya kupata baraka kubwa zaidi maishani.

“Ni Mwenye Upendo Mwororo Sana”

Yehova alikuwa “mwenye upendo mwororo sana na mwenye rehema” kwa Ayubu. (Yakobo 5:11) Jinsi gani? Yehova alimrudishia Ayubu afya nzuri. Wazia jinsi alivyohisi alipoona kwamba, kwa kweli, mwili wake ulikuwa “na afya zaidi kuliko wakati wa ujana” kama Elihu alivyotabiri! Mwishowe alizungukwa na familia na rafiki zake, waliomwonyesha huruma na kumpa zawadi. Yehova alimrudishia Ayubu mali yake, na kumpa mara mbili ya mali aliyokuwa nayo mwanzoni. Namna gani majeraha makali zaidi—kufiwa na watoto wake? Ayubu na mke wake walifarijiwa kwa kupata watoto wengine kumi! Na Yehova akarefusha kimuujiza uhai wa Ayubu. Ayubu aliishi miaka 140 zaidi, muda uliomtosha kuona vizazi vinne vya watoto wake. Kisha Biblia inasema, “Mwishowe Ayubu akafa, baada ya kuishi maisha marefu na yenye kuridhisha.” (Ayubu 42:10-17) Katika Paradiso, Ayubu na mke wake mpendwa wataungana tena na familia yao, kutia ndani watoto wao ambao Shetani aliwaua.—Yohana 5:28, 29.

Kwa nini Yehova alimbariki sana Ayubu? Biblia inajibu hivi: “Mmesikia kuhusu uvumilivu wa Ayubu.” (Yakobo 5:11) Ayubu alivumilia matatizo ambayo wengi wetu hatujakabili. Neno “uvumilivu” linaonyesha kwamba Ayubu hakukabiliana tu na majaribu hayo. Aliendelea kuvumilia kwa imani na upendo kwa Yehova. Badala ya kuwa na uchungu na kukasirika, aliendelea kuwa tayari kuwasamehe hata wale waliomuumiza kimakusudi. Na hakuacha kamwe tumaini lake lenye thamani na kitu chenye thamani zaidi maishani mwake, yaani, utimilifu wake.—Ayubu 27:5.

Kila mmoja wetu anahitaji uvumilivu. Tuna hakika kwamba Shetani atajaribu kutuvunja moyo kama alivyofanya kwa Ayubu. Lakini, tukiendelea kuvumilia kwa imani, kuwa wanyenyekevu, kuwa tayari kuwasamehe wengine, na kuazimia kulinda utimilifu wetu, sisi pia tutaendelea kushikilia tumaini letu lenye thamani. (Waebrania 10:36) Tukimwiga Ayubu tutamkasirisha sana Shetani, hata hivyo, tutaufurahisha moyo wenye upendo wa Yehova!

^ fu. 6 Elifazi, Bildadi, na Sofari walimwambia Ayubu maneno mengi sana—yaliyotosha kujaza sura tisa za Biblia—hata hivyo, hakuna sehemu yoyote ambayo walimwita Ayubu kwa jina.

^ fu. 14 Nyakati nyingine, Yehova anafafanua mambo kwa njia iliyo wazi, kisha anatumia maneno ya mfano au ya kishairi. (Kwa mfano, tazama, Ayubu 41:1, 7, 8, 19-21.) Katika pindi zote, kusudi la Mungu lilikuwa lilelile—kumsaidia Ayubu astaajabishwe na Muumba wake.

^ fu. 18 Baadaye, mtume Paulo alisema maneno ya Elifazi, akiyanukuu kama ukweli. (Ayubu 5:13; 1 Wakorintho 3:19) Elifazi alisema ukweli, lakini hakuufafanua kwa njia sahihi kuhusiana na Ayubu.

^ fu. 19 Hakuna sehemu yoyote inayoonyesha kwamba Ayubu alipaswa kutoa dhabihu kama hiyo kwa niaba ya mke wake.