Hamia kwenye habari

Dada Hermine Schmidt

APRILI 18, 2024
UJERUMANI

Hermine Schmidt, Shahidi wa Mwisho Anayejulikana Kuokoka Katika Kambi za Mateso za Wanazi Amekufa Akiwa na Umri wa Miaka 98

Hermine Schmidt, Shahidi wa Mwisho Anayejulikana Kuokoka Katika Kambi za Mateso za Wanazi Amekufa Akiwa na Umri wa Miaka 98

Hermine kabla hajapelekwa kwenye kambi ya mateso ya Stutthof

Machi 31, 2024, Dada Hermine Schmidt alikufa akiwa na umri wa miaka 98. Yeye ndiye wa mwisho kati ya Mashahidi wa Yehova ambao waliteswa katika kambi za mateso za Wanazi kwa sababu ya imani yao.

Hermine alizaliwa Novemba 13, 1925, katika jiji la Gdańsk, ambalo kwa sasa ni sehemu ya Poland. Wazazi wake, Oskar na Frieda Koschmieder, walikuwa Mashahidi wa Yehova. Walimsaidia binti yao kusitawisha imani yenye nguvu na kumtumaini Yehova. Mwaka wa 1939, jeshi la Wanazi liliteka eneo la Gdańsk, na mateso makali dhidi ya Mashahidi wa Yehova yakaanza. Wakati huo, Hermine alijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa Mei 2, 1942, akiwa na umri wa miaka 16.

Mwaka uliofuata, Juni 1943, Wanazi walimkamata na kumfunga Hermine akiwa na umri wa miaka 17. Alikamatwa mara ya pili mwezi wa Aprili 1944, na wakati huo alipelekwa kwenye kambi ya mateso ya Stutthof. Akifikiria wakati huo mbaya, pindi moja Hermine alisema: “Si rahisi kukabiliana na hali iliyotokea. Tuliteswa na kuumizwa vibaya sana. Askari wa Nazi walifanya yote waliyoweza ili kunivunja moyo. Sikuzaliwa nikiwa shujaa. Nilikuwa msichana wa kawaida tu. Lakini sikuwa na shaka yoyote akilini mwangu kuhusu kile nilichopaswa kufanya. Hilo lilihusu ushikamanifu wangu na kutenda kupatana na dhamiri yangu. Unapotenda kupatana na dhamiri yako unapata amani—amani yako binafsi na pia unapata amani pamoja na Mungu.”

Horst na Hermine mwezi Machi 1995

Mwaka mmoja baadaye, mwezi wa Aprili 1945, jeshi la Urusi lilikaribia kambi ya Stutthof. Walinzi wa SS wa Ujerumani waliwalazimisha wafungwa wengi waingie kwenye mashua na wakawaacha baharini badala ya kuruhusu wakombolewe na jeshi la Urusi. Hermine na wengine 370 waliokolewa mashua yao ilipoyumbishwa hadi kwenye kisiwa cha Denmark cha Møn mwezi Mei 1945. Muda mfupi baada ya hapo, Hermine aliungana tena na wazazi wake.

Mwaka wa 1947, Hermine alifunga ndoa na Horst Schmidt. Horst alikataa kutumikia jeshini na pia alifanya kazi ya kusafirisha machapisho kisiri wakati kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipokuwa chini ya marufuku. Alishtakiwa, akahukumiwa kifo, na akafungwa katika gereza la Brandenburg-Görden. Alikombolewa Aprili 27, 1945, muda mfupi kabla ya muda ambao angeuawa. Horst na Hermine walikuwa wenzi wa ndoa kwa karibu miaka 63 hadi Horst alipokufa mwaka wa 2010.

Akina Schmidt walitumia miaka mingi wakizungumza na watu kuhusu mambo waliyokabili maishani. Katika mahojiano yaliyofanyika mwaka wa 1998, Hermine alizungumzia kuhusu maisha yake ya ushikamanifu kwa Yehova: “Maisha haya hayajakuwa rahisi kwangu , lakini ndiyo maisha bora zaidi. Siwezi kuyabadili na chochote kile.”

Tunathamini sana mfano wa Hermine wa ushikamanifu alipokabili majaribu. Na tuige imani yake kwa kuazimia kuonyesha ujasiri na kuufanya moyo wetu uwe imara, tukiwa na uhakika kwamba siku zote Yehova atawalinda washikamanifu wake.​—Zaburi 31:23, 24.