Hamia kwenye habari

April 2024 ni mwaka wa 75 tangu gazeti Mnara wa Mlinzi lianze kuchapishwa katika Kisebuano (kushoto) na Kipangasinani (kulia)

APRILI 3, 2024
FILIPINO

Miaka Sabini na Tano Tangu Kuanza Kuchapishwa kwa Gazeti Mnara wa Mlinzi Katika Kisebuano na Kipangasinani

Miaka Sabini na Tano Tangu Kuanza Kuchapishwa kwa Gazeti Mnara wa Mlinzi Katika Kisebuano na Kipangasinani

Aprili 2024 tulikumbuka tukio muhimu la kuanza kutokeza machapisho yanayotegemea Biblia nchini Filipino. Miaka sabini na tano iliyopita, Aprili 1949, Mnara wa Mlinzi lilipatikana kwa mara ya kwanza katika lugha za Kisebuano na Kipangasinani.

Kazi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme nchini Filipino ilianza mwanzoni mwa miaka ya 1900. Mwanzoni ndugu na dada zetu walitumia machapisho ya Kiingereza katika huduma, lakini ilionekana wazi kwamba tulihitaji kuwa na machapisho katika lugha za wenyeji. Kuanzia mwaka wa 1947, jitihada zilifanywa ili kuanza kutafsiri Mnara wa Mlinzi katika Kitagalogi, lugha inayozungumzwa na watu wengi zaidi nchini Filipino. Kisha mwishoni mwa 1948, mipango ilifanywa ili kutafsiri Mnara wa Mlinzi katika Kisebuano na Kipangasinani. Miezi michache baada ya hapo, matoleo ya kwanza yalichapishwa.

Nakala ya Mnara wa Mlinzi katika Kipangasinani kuanzia mwaka wa 1949

Kwa miaka miwili iliyofuata, ndugu na dada zetu walitumia mashine ndogo zilizoendeshwa kwa mikono ili kutokeza machapisho kwenye ofisi ya tawi. Kwa kuwa uhitaji wa magazeti uliongezeka, uchapishaji wa Mnara wa Mlinzi katika Kisebuano na Kipangasinani ulihamishiwa kwenye Makao Makuu ya Ulimwenguni Pote ya Mashahidi wa Yehova, yaliyokuwa Brooklyn, New York, Marekani. a

Ndugu Juan Landicho

Baadhi ya wale walioshiriki kutafsiri Mnara wa Mlinzi katika Kisebuano na Kipangasinani waliliona kuwa pendeleo kushiriki katika kazi hiyo ya kutafsiri. Ndugu Juan Landicho, ambaye alifanya kazi ya kutafsiri katika timu ya Kipangasinani miaka ya 1980, anakumbuka: “Mwanzoni gazeti la Mnara wa Mlinzi katika Kipangasinani, lilitolewa miezi sita baada ya toleo la Kiingereza kwa sababu ya kuchelewa katika kazi ya kutafsiri. Tulifurahi sana mwaka wa 1986, ambapo maboresho yalifanywa katika mbinu za kutafsiri na hilo likasaidia kupata toleo la kiingereza na la Kipangasinani kwa wakati uleule mmoja. Kwa kweli tulijionea Yehova akibariki jitihada zetu kupitia roho yake takatifu.”

Vivyo hivyo, Dada Belen Cañete, anayetumikia katika ofisi ya tawi ya Filipino amesaidia katika kazi ya kutafsiri machapisho yanayotegemea Biblia katika Kisebuano kwa muda wa miaka 46, anasema hivi: “Mwanzoni tulikuwa na watafsiri wachache tu, na kulikuwa na kazi nyingi ya kufanya. Pindi nyingine haikuwa rahisi kufanya kazi hiyo. Lakini sasa tuna ndugu na dada waliozoezwa vizuri, teknolojia ya kisasa na tuna kila kitu tunachohitaji ili kufanya kazi hii. Kwa kweli nimejionea jinsi ambavyo Yehova amebadili shaba kuwa dhahabu na kuhakikisha kwamba watumishi wake wanatunzwa vizuri.”

Timu ya utafsiri ya Kipangasinani (kushoto) na Kisebuano (kulia)

Zaidi ya watu milioni 26 nchini Filipino wanazungumza Kisebuano, kutia ndani ndugu na dada zetu zaidi ya 76,000 wanaotumikia katika makutaniko 1,150 ya lugha ya Kisebuano. Kwa kuongezea, miongoni mwa karibu watu milioni 2 wanaozungumza Kipangasinani kuna ndugu na dada zetu 6,000 hivi wanaotumikia katika makutaniko 68 ya lugha ya Kipangasinani. Kwa ujumla, ofisi ya tawi ya Filipino inasimamia kazi ya kutafsiri machapisho katika lugha 24. Mnara wa Mlinzi unachapishwa katika lugha kumi kati ya lugha hizo kila mwezi. Kwa sasa ofisi ya tawi ya Japani inasimamia uchapishaji wa Machapisho yanayotegemea Biblia katika Kisebuano na Kipangasinani.

Tunashukuru sana kwamba Yehova amebariki jitihada hizo za utafsiri, na amefanya ujuzi kuhusu Neno lake upatikane kwa watu walio na kiu ya kweli wanaozungumza Kisebuano na Kipangasinani!—Isaya 55:1.

a Leo Makao Makuu ya Mashahidi wa Yehova yako Warwick, New York, Marekani.