Hamia kwenye habari

Familia ya Betheli ikiwasalimu wageni wanapowasili kwa ajili ya kuweka wakfu majengo mapya ya ofisi ya tawi ya Argentina

APRILI 22, 2024
ARGENTINA

Majengo Mapya ya Ofisi ya Tawi Yamewekwa Wakfu Nchini Argentina

Majengo Mapya ya Ofisi ya Tawi Yamewekwa Wakfu Nchini Argentina

Ndugu Winder akitoa hotuba ya wakfu

Aprili 6, 2024, majengo mapya ya ofisi ya tawi yaliyo Buenos Aires, nchini Argentina, yaliwekwa wakfu wakati wa hotuba iliyotolewa na Ndugu Jeffrey Winder, mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Karibu ndugu na dada 500 walihudhuria programu hiyo ya wakfu katika kumbi tatu za majengo mapya ya Betheli. Wahudhuriaji wengine 5,844 waliunganishwa katika programu hiyo kupitia video mtandaoni wakiwa kwenye Jumba la Makusanyiko karibu na jiji la Ezeiza. Siku iliyofuata, mkutano wa pekee ulifanyika kwenye Jumba la Makusanyiko na kupeperushwa kwenye makutaniko yote yaliyo Argentina na Uruguai, na jumla ya watu 181,643 walihudhuria.

Mipango ilifanywa ili wageni watembelee majengo hayo mapya ya ofisi ya tawi, wafurahie ushirika mchangamfu, na kushiriki katika utendaji mwingine wa pekee. Miongoni mwao kulikuwa na zaidi ya ndugu na dada 230 kutoka mataifa 25. Ndugu Sergio Spaccasassi, ambaye kwa sasa anatumikia nchini Ekuado, alisaidia katika kazi ya ujenzi wa ofisi mpya ya tawi nchini Argentina. Akiwarejelea watu kutoka mataifa mbalimbali ambao walihudhuria programu hiyo ya wakfu alisema hivi: “Yehova anatumia pindi za pekee kama hizi ili kutuleta pamoja tukiwa familia ya waabudu wake.”

Ndugu Juan Carlos Nigro, mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Argentina, anasema: “Tulijionea jinsi ambavyo Yehova aliongoza na kubariki kila hatua ya mradi huu. Yeye ndiye ametuandalia jengo hili ambalo linaleta heshima kwa jina lake.”

Ndugu na dada wakifurahia programu ya wakfu wakiwa kwenye ukumbi wa majengo mapya ya Betheli yaliyo Buenos Aires

Pamoja na ndugu na dada zetu nchini Argentina, tunamshukuru sana Yehova, ambaye “amefanya kila kitu kipendeze kwa wakati wake,” kwa ajili ya mjengo haya mapya ya Betheli.—Mhubiri 3:11.