Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Nitaweza Kweli Kuwasaidia Watu Hawa?

Je, Nitaweza Kweli Kuwasaidia Watu Hawa?

Barua Kutoka Benin

Je, Nitaweza Kweli Kuwasaidia Watu Hawa?

ILIKUWA asubuhi moja katika inchi ya Afrika ya Mangaribi. Harufu ya michuzi na wali inayotokota kwenye moto ilienea katika hewa. Wanawake walitembea wakiwa na mizigo mikubwa juu ya vichwa vyao bila kuishikilia. Sauti za watu waliokuwa wakicheka zilichanganyika na sauti za watu waliokuwa wakibishana bei ya vitu. Jua lilikuwa tayari kali sana ingawa ilikuwa bado asubuhi.

Kwa kuona tu Yovo, ao muzungu, kikundi cha watoto walianza kuimba na kucheza wimbo wao ambao walizoea. Wimbo huo ulianza kwa maneno “Yovo, Yovo, bon soir” na ulimalizika kwa maneno “Je, hakuna zawadi kisha kukuimbia?” Kijana mumoja hakuwa anaimba. Nilipoendelea na safari yangu, alinifuata na akaanza kufanya ishara kwa mikono yake. Hiyo ilionekana kama Luga ya Ishara. Katika États-Unis, nilijifunza kuzungumuza Luga ya Ishara ya Amerika, lakini Benin ni inchi inayozungumuza Kifaransa.

Nilijikaza kufanya ishara ya herufi munane zinazounda jina langu. Kijana huyo alionyesha sura ya kicheko. Alinishika mukono na akanielekeza katika njia nyembamba zinazoongoza mupaka kwenye nyumba yao, ambayo ilikuwa na vyumba viwili na iliyojengwa kwa motofali mabichi. Watu wa familia yake walikuja wote na kunizunguka. Kila mutu alikuwa anafanya Luga ya Ishara. Sasa ningefanya nini? Nilifanya ishara ya jina langu na kisha niliandika barua ndogo iliyosema kwamba nilikuwa misionere anayefundisha Biblia na kwamba ningerudi tena. Majirani fulani ambao hawakuwa viziwi walijiunga na sisi, na wote walitikisa vichwa ili kukubali nirudi tena. Niliwaza hivi: “Je, nitaweza kweli kuwasaidia watu hawa?”

Niliporudi nyumbani nilifikiri, ‘Ni lazima mutu fulani awasaidie watu hawa wajifunze juu ya ahadi hii ya Mungu: “Masikio ya viziwi yatazibuliwa.”’ (Isaya 35:5) Nilifanya utafiti fulani. Uchunguzi uliofanywa hivi karibuni ulionyesha kwamba katika inchi ya Benin hesabu ya viziwi na watu ambao hawasikie vizuri ilifikia 12000. Nilifurahi sana niliposikia kwamba ni Luga ya Ishara ya Amerika ndiyo iliyofundishwa katika masomo ya viziwi, wala si Luga ya Ishara ya Ufaransa. Lakini nilihuzunika kujua kwamba hakuna Shahidi wa Yehova hata mumoja aliyejua Luga ya Ishara ya Amerika. Kwa sikitiko, nilimuambia Shahidi wa Yehova mumoja hivi: “Ningefurahi ikiwa mutu fulani anayejua Luga ya Ishara ya Amerika angekuja na kusaidia.” Shahidi huyo alinijibu hivi: “Wewe uko hapa, unaweza kuwasaidia, sivyo?” Alikuwa na haki ya kusema hivyo! Nilifanya ombi la DVD fulani za Luga ya Ishara ya Amerika zilizotolewa na Mashahidi wa Yehova na pia kitabu cha kunisaidia nijifunze mimi mwenyewe Luga ya Ishara. Sala zangu za kuomba musaada zilijibiwa wakati Shahidi mumoja aliyejua Luga ya Ishara ya Amerika alipotoka Cameroun na kuhamia Benin.

Watu wengi walisikia kama nilikuwa ninajifunza Luga ya Ishara. Niliambiwa kwamba ninapaswa kumutembelea Brice, ambaye alikuwa fundi wa kuchora sanamu kwenye vibao. Kibanda chake ambamo alifanyia kazi kilijengwa na majani ya mungazi yaliyosukwa-sukwa na kilikuwa na hewa ya baridi wakati wa joto. Kwa muda wa miaka mingi, kuta za kibanda chake zilingarishwa kwa rangi mbalimbali kama rangi za upinde wa mvua. Alipanguza vumbi juu ya viti viwili na akaanza kuniangalia, akingojea nianzishe mazungumuzo. Niliingiza DVD ndani ya mashini ndogo ya kucheza DVD. Alisogeza kiti chake karibu na mashini hiyo. Mwanaume huyo akasema kwa Luga ya Ishara hivi: “Ninaelewa, ninaelewa!” Watoto wengi wa majirani walikuja na wakainamisha shingo zao ili kuona. Mumoja wa watoto hao akasema kwa sauti: “Sababu gani wanaangalia filme ambayo haina sauti?”

Kila mara nilipoenda kumuona Brice, watu wengi sana walikusanyika hapo ili kuangalia DVD. Kisha muda kidogo Brice na wengine wakaanza kuja kwenye mikutano yetu ya kutaniko. Kujikaza kuwatafsiria katika Luga ya Ishara kulinisaidia nijue haraka zaidi luga hiyo. Kikundi hicho cha Luga ya Ishara kilipoongezeka, wengine kati yao walianza hata kuja kunitafuta nyumbani. Kwa mufano, siku moja motokari yangu iliyozeeka ilikoroma​-koroma ilipokwama ndani ya mashimo nilipojaribu kuepuka kugonga mbuzi na nguruwe zilizokuwa zikitembelea​-tembea. Halafu kwa gafula nilisikia mutu akigonga nyuma ya motokari yangu. Aah, nilifikiri kwamba motokari imeharibika tena! Lakini haikuwa kama nilivyofikiri, ilikuwa ni kiziwi aliyekuwa anakimbia nyuma ya motokari yangu na kujaribu kuniita kwa kugonga​-gonga nyuma ya motokari yangu!

Vikundi vya Luga ya Ishara ya Amerika vilianzishwa katika miji mingine. Mupango wa kutafsiri vipindi mbalimbali vya mukusanyiko wa wilaya wa kila mwaka katika Luga ya Ishara ulipoanza, nilikuwa kati ya wale ambao waliombwa kutafsiri katika luga hiyo. Nilipopanda kwenye jukwaa na kungojea musemaji aanze hotuba yake, kwa muda kidogo nilikumbuka wakati ule nilipoanza kutumika katika mugawo wangu. Nilikuwa ninajiuliza hivi: “Ninaweza kufanya nini zaidi nikiwa misionere katika Afrika?” Nilipowaangalia wasikilizaji, nilijua kwamba nilikuwa nimekwisha kupata jibu, ni kusema, ninapaswa kuwa misionere anayesaidia viziwi. Sijiulize tena hivi: “Je, nitaweza kweli kuwasaidia watu hawa?”