Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Wafundishe Watoto Wako Maadili Mema

Wafundishe Watoto Wako Maadili Mema

Siri ya Furaha ya Familia

Wafundishe Watoto Wako Maadili Mema

Loida, * mama kutoka Mexico, anasema: “Vijana wanapewa kondomu shuleni na hivyo kuwafanya wafikiri kwamba si vibaya kufanya ngono—bora tu wahakikishe ngono hiyo ni ‘salama.’”

Nobuko, mama kutoka Japani, anasema: “Nilimuuliza mwana wangu angefanya nini kama angejikuta akiwa peke yake pamoja na rafiki yake wa kike? Naye akanijibu, ‘Sijui.’”

MWANA au binti yako alipokuwa mtoto mdogo, je, ulihakikisha kwamba nyumba yako ni salama? Labda ulifunika swichi za umeme, ukaficha vifaa vyenye ncha kali, na kuweka vizuizi kwenye ngazi. Ulifanya yote hayo ili mtoto wako awe salama.

Laiti ingekuwa rahisi hivyo kumlinda mtoto wako aliyefikia umri wa kubalehe! Sasa una wasiwasi hata zaidi, unafikiria: ‘Je, mwana wangu anatazama au kusoma habari chafu kuhusu ngono?’ ‘Je, binti yangu anatuma picha zake chafu kupitia simu ya mkononi?’ Na swali linalotia wasiwasi hata zaidi ni, ‘Je, kijana wangu ameanza kufanya ngono?’

Kujaribu Kuwadhibiti Vijana Si Suluhisho

Baadhi ya wazazi hujaribu kuwadhibiti vijana wao kwa kuchunguza kila kitu wanachofanya. Baadaye, wazazi hao hugundua kwamba kujaribu kuwadhibiti vijana kwa njia hiyo, kunawafanya wafiche kila kitu ambacho wazazi wao wamewakataza wasifanye.

Bila shaka, kumdhibiti kijana wako si suluhisho. Yehova Mungu mwenyewe hatumii njia hiyo ili kuwafanya viumbe wake wamtii, nawe hupaswi kufanya hivyo ukiwa mzazi. (Kumbukumbu la Torati 30:19) Hivyo, unaweza kuwasaidia vijana wako jinsi gani kufanya maamuzi ya kimaadili yenye hekima?—Methali 27:11.

Hatua ya msingi ni kuzungumza na watoto wako kila mara na kuanza kufanya hivyo wakiwa bado wadogo. * (Methali 22:6) Kisha, wanapofikia umri wa kubalehe, endelea kuzungumza nao. Ukiwa mzazi, unapaswa kuwa chanzo cha habari chenye kutegemeka. Alicia, msichana kutoka Uingereza anasema, “Watu wengi hufikiri kuwa tungependelea kuzungumza kuhusu ngono na rafiki zetu, lakini hilo si kweli. Tunathamini sana habari hizo zinapotoka kwa wazazi wetu. Tunaamini yale wanayotuambia.”

Uhitaji wa Kuwa na Maadili Mema

Watoto wanapoendelea kukua, wanahitaji kujua mambo mengi zaidi kuhusu ngono kuliko kujua tu mambo ya msingi kuhusu jinsi uhai unavyotokea. Pia, ‘nguvu zao za ufahamu zinapaswa kuzoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa.’ (Waebrania 5:14) Kwa ufupi, wanahitaji kujua kinachomaanishwa na maadili mema na kwamba wanapaswa kuishi kulingana na maadili hayo. Unaweza kumfundisha maadili mema kijana wako jinsi gani?

Anza kwa kuchunguza maadili yako mwenyewe. Kwa mfano, huenda ukaamini kwamba uasherati, yaani, ngono kati ya watu ambao hawajafunga ndoa ni mbaya. (1 Wathesalonike 4:3) Huenda watoto wako wanajua msimamo wako kuhusu jambo hilo; wanaweza pia kunukuu maandiko yanayounga mkono msimamo wako. Wanapoulizwa, huenda wakasema bila kusita kwamba ngono kabla ya ndoa ni mbaya.

Lakini wanahitaji kujua mengi zaidi. Kitabu Sex Smart kinadokeza kuwa baadhi ya vijana wanaweza kusema tu kwamba wanaunga mkono maoni ya wazazi wao kuhusu ngono. Kitabu hicho kinasema: “Wanasita kuwa na maoni yao wenyewe. Wanapojikuta katika hali wasiyotazamia na kulazimika kuamua kati ya mwenendo unaofaa na usiofaa, wanachanganyikiwa wasijue la kufanya.” Hiyo ndio sababu ni muhimu sana kuwa na viwango vya maadili. Unaweza kumsaidia kijana wako jinsi gani asitawishe viwango hivyo?

Eleza waziwazi viwango vyako vya maadili. Je, unaamini kwamba ngono inapaswa kufurahiwa tu na wale waliofunga ndoa? Basi, mweleze kijana wako waziwazi na kwa ukawaida. Kulingana na kitabu Beyond the Big Talk, utafiti unaonyesha kwamba “katika familia ambazo wazazi wanawaeleza vijana wao waziwazi kwamba hawataki wajihusishe na ngono, kuna uwezekano wa vijana hao kutojiingiza katika ngono mapema.”

Bila shaka, kama ilivyotajwa mapema, kumweleza tu mwana au binti yako kuhusu viwango vyako vya maadili hakumaanishi kwamba ataishi kulingana na viwango hivyo. Hata hivyo, kueleza waziwazi kuhusu viwango vya maadili ambavyo ungetaka familia yako iwe navyo, ni jambo linaloweza kuwasaidia watoto wasitawishe maadili mema. Uchunguzi umeonyesha kwamba hatimaye vijana wengi hufuata viwango vya maadili vya wazazi wao hata ingawa walionekana kuvipuuza mwanzoni.

JARIBU KUFANYA HIVI: Tumia tukio fulani lililotajwa kwenye vyombo vya habari kuanzisha mazungumzo na kueleza kuhusu viwango vyako vya maadili. Kwa mfano, ikiwa uhalifu unaohusu ngono unatajwa, unaweza kusema: “Mimi huchukizwa na jinsi wanaume fulani wanavyojaribu kuwatumia wanawake vibaya. Unafikiri wanapata maoni hayo wapi?”

Wafundishe ukweli wote kuhusu ngono. Maonyo ni muhimu. (1 Wakorintho 6:18; Yakobo 1:14, 15) Hata hivyo, Biblia inaitaja ngono kuwa zawadi kutoka kwa Mungu, bali si mtego wa Shetani. (Methali 5:18, 19; Wimbo wa Sulemani 1:2) Kuwaeleza vijana wako kuhusu tu hatari za kufanya ngono, kunaweza kuwaacha na mtazamo uliopotoka na usio wa Kimaandiko kuihusu. Mwanamke mmoja kijana aitwaye Corrina kutoka Ufaransa anasema, “Wazazi wangu walikazia tu mwenendo mpotovu kingono na hilo lilinifanya niwe na mtazamo mbaya kuhusu ngono.”

Hakikisha kwamba unawaeleza watoto wako ukweli wote kuhusu ngono. Mama mmoja nchini Mexico aitwaye Nadia, anasema, “Kile ambacho wakati wote nimejaribu kuwaeleza vijana wangu ni kwamba ngono ni nzuri na ni jambo la kawaida, na kwamba Yehova Mungu aliwapa wanadamu ili waifurahie. Lakini inapaswa kufurahiwa tu katika ndoa. Ngono inaweza kutuletea furaha au mateso, ikitegemea jinsi tunavyoitumia.”

JARIBU KUFANYA HIVI: Pindi nyingine unapozungumza na kijana wako kuhusu ngono, malizia mazungumzo kwa njia nzuri. Usiogope kumweleza kwamba ngono ni zawadi nzuri kutoka kwa Mungu na kwamba anaweza kuifurahia baadaye akifunga ndoa. Onyesha kwamba una hakika kuwa kijana wako ataendelea kufuata viwango vya Mungu hadi wakati huo.

Msaidie kijana wako afikirie matokeo ya maamuzi yake. Ili kufanya maamuzi mazuri katika maisha, vijana wanahitaji kujua mambo mbalimbali wanayoweza kuchagua kufanya na kuchunguza uzuri na ubaya wa kila jambo. Usifikiri kuwa inatosha kwa watoto wako kujua tu lililo sawa na lisilo sawa. “Nikikumbuka makosa niliyoyafanya ujanani,” anasema mwanamke Mkristo nchini Australia aitwaye Emma, “ninaweza kusema kwamba kujua tu kanuni za Mungu hakumaanishi kuwa unakubaliana nazo. Ni muhimu kujua manufaa ya kanuni hizo na matokeo ya kuzivunja.”

Biblia inaweza kutusaidia, kwa sababu amri nyingi zinazopatikana humo zimeambatanishwa na maneno yanayoonyesha waziwazi matokeo ya kufanya mambo mabaya. Kwa mfano, andiko la Methali 5:8, 9 linawahimiza vijana waepuke uasherati ‘ili wasije wakawapa wengine heshima yao.’ Kama mistari hiyo inavyoonyesha, ngono kabla ya ndoa inaathiri sifa nzuri za mtu, inamzuia asimtumikie Mungu kwa ukamili, na kufanya asijiheshimu. Na hilo hufanya iwe vigumu kwa yeyote mwenye sifa nzuri kuvutiwa na mtu kama huyo kuwa mwenzi wake wa ndoa. Kufikiria madhara ya kimwili, kihisia, na kiroho yanayotokana na kupuuza sheria za Mungu kunaweza kumsaidia kijana wako aazimie kuishi kulingana na sheria hizo. *

JARIBU KUFANYA HIVI: Tumia mifano kumsaidia kijana wako aone hekima ya kanuni za Mungu. Kwa mfano, unaweza kusema: “Moto wa kupikia ni mzuri; lakini moto unaoteketeza msitu ni mbaya. Kuna tofauti gani kati ya mambo hayo, na jibu lako linahusiana jinsi gani na mipaka ambayo Mungu ameweka kuhusiana na ngono?” Tumia simulizi linalopatikana katika Methali 5:3-14 kumsaidia kijana wako aelewe matokeo mabaya ya kufanya uasherati.

Takao, mwenye umri wa miaka 18 kutoka nchini Japani, anasema, “Ninajua kwamba ninapaswa kufanya yaliyo sawa, lakini inanibidi kuendelea kupambana na tamaa za mwili.” Vijana wanaopambana na hali kama hiyo wanaweza kufarijika kujua kwamba hawako peke yao. Hata mtume Paulo, aliyekuwa Mkristo thabiti, alikiri hivi: “Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.”—Waroma 7:21.

Ingefaa vijana watambue kwamba pambano kama hilo si baya. Linaweza kuwachochea wafikirie wanataka kuwa watu wa aina gani. Hilo linaweza kuwasaidia wafikirie kwa uzito swali hili: ‘Je, ninataka kuongoza maisha yangu na hivyo kujulikana kuwa mtu mwenye sifa nzuri na thabiti, au ninataka kujulikana kuwa mtu anayeongozwa tu na tamaa zake?’ Ikiwa kijana wako ana viwango vizuri vya maadili, hilo litamsaidia kujibu swali hilo kwa hekima.

[Maelezo ya Chini]

^ Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ Ili kupata mapendekezo kuhusu jinsi ya kuanzisha mazungumzo pamoja na watoto wako kuhusu ngono, na jinsi unavyoweza kutumia mapendekezo hayo kulingana na umri wao, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 1, 2010 (1/11/2010), uku. 12-14.

^ Kwa habari zaidi, ona makala “Vijana Huuliza . . . Je, Ngono Itaboresha Uhusiano Wetu?” katika gazeti la Amkeni! la Aprili (Mwezi wa 4) 2010 lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

JIULIZE . . .

▪ Nina uthibitisho gani kwamba kijana wangu anafuata viwango thabiti vya maadili?

▪ Ninapozungumza na kijana wangu kuhusu ngono, je, ninamweleza kwamba hiyo ni zawadi kutoka kwa Mungu au ni mtego wa Shetani?

[Sanduku katika ukurasa wa 20]

Mwongozo wa Biblia Unafaa Hata Leo

“Kwa miaka mingi mwongozo kuhusu ngono unaopatikana katika Biblia, umethibitika kuwa wenye manufaa. Nyakati hizi ambapo vijana wanaathirika sana kihisia kwa kufanya ngono kabla ya ndoa, kupata mimba nje ya ndoa, kupatwa na magonjwa kama UKIMWI na mengine yanayoambukizwa kingono, shauri la Kimaandiko kwamba ngono inapaswa kufanywa katika kifungo cha ndoa . . . linafaa kabisa, na hiyo ndio ‘ngono pekee iliyo salama’ na inayofaa.”—Parenting Teens With Love and Logic.