Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MUSAADA KWA FAMILIA | VIJANA

Namna ya Kupambana na Hali ya Kujisikia Kuwa Peke Yako

Namna ya Kupambana na Hali ya Kujisikia Kuwa Peke Yako

TATIZO

“Nilikuwa na marafiki wawili wanawake wenye walikuwa wanafanya mambo pamoja bila mimi. Kila mara nilisikia kama walikuwa wanapitisha wakati muzuri sana pamoja. Siku moja niliita kwenye namba ya telefone ya nyumbani kwa mumoja wao; yule mwengine pia alikuwa katika nyumba hiyo, na wakati mutu mwengine alijibia kwenye telefone, nilisikia sauti ya hao marafiki wangu wanaongea na kucheka. Niliweza tu kusikia namna walikuwa wanajifurahisha, na hilo lilifanya nijisikie zaidi kuwa peke yangu kuliko namna nilikuwa!”—Maria. *

Kuna siku umejisikia kama wengine wamekuacha ao kama uko peke yako? Ikiwa ni hivyo, Biblia inatoa mashauri yenye inaweza kukusaidia. Kwanza kabisa, fikiria mambo fulani yenye unapaswa kujua juu ya hali ya kujisikia kuwa peke yako.

MAMBO UNAPASWA KUJUA

Karibu kila mutu anajisikia kuwa peke yake wakati fulani. Hata watu wenye wanaonekana kuwa wanajulikana sana wanajisikia pia hivyo. Sababu gani? Kwa sababu mara nyingi jambo lenye linaonyesha ikiwa mutu anajisikia kuwa peke yake ao hapana, haiko hesabu ya marafiki wake lakini ni aina ya urafiki wake pamoja na wengine. Mutu mwenye kujulikana sana anaweza kuwa kila mara pamoja na watu wengi lakini bila kuwa na marafiki wa kweli, na hilo linamufanya ajisikie kuwa peke yake.

Kujisikia kuwa peke yako kunaweza kuwa hatari kwa afya yako. Watu fulani wenye elimu walijifunza matokeo ya uchunguzi 148 wenye ulifanywa, na wakasema kama kukosa kuwa karibu na wengine kunaweza kufanya mutu akufe mbio, na kwamba jambo hilo ni lenye “hatari mara mbili kuliko hatari ya kunenepa sana” na “linalingana na kuvuta tumbako 15 kila siku.”

Kujisikia kuwa peke yako kunaweza kukufanya ukubali marafiki wabaya. Kwa kweli, hali hiyo inaweza kukufanya ukubali kila mutu mwenye anapenda kufanya urafiki na wewe. Kijana mumoja mwanaume anayeitwa Alan anasema hivi: “Wakati mutu anajisikia kuwa peke yake, anatamani sana kupata mutu wa kumuhangaikia. Unaweza kuanza kuwaza kama ni muzuri mutu yeyote akuhangaikie kuliko kukosa hata mutu mumoja wa kukuhangaikia. Na jambo hilo linaweza kukuletea magumu.”

Teknolojia haimalize sikuzote tatizo la kujisikia kuwa peke yako. Kijana mumoja mwanamuke anayeitwa Natalie anasema hivi: “Kwa siku moja, ningeweza kuandikia hata watu mia moja ujumbe kwenye telefone ao kwenye Internete, lakini niliendelea kujisikia sana kuwa peke yangu.” Kijana mwengine mwanaume anayeitwa Tyler anaunga mukono mawazo hayo. Anasema hivi: “Kutuma ujumbe ni kama kula chakula chepesi kama vile ndazi, lakini kuonana na mutu ni kama kula chakula cha kweli-kweli. Vyakula vyepesi ni vitamu, lakini ili ushibe ni lazima ukule chakula cha kweli-kweli.”

MAMBO UNAWEZA KUFANYA

Ukuwe na mawazo mazuri. Kwa mufano, tuseme unafungua adresi fulani ya Internete ya kutumiana picha, na unaona picha za marafiki wako kwenye tukio fulani ambako haukualikwa. Wakati huo uamuzi ni wako; ukipenda unaweza kuwaza kama walikosa kukualika kimakusudi ao unaweza kuwa na mawazo mazuri. Kwa sababu hauwezi kujua mambo yote yenye yalifanya usialikwe, sababu gani ukuwe na mawazo mabaya? Kuliko kuwa na mawazo hayo, ujikaze kufikiria ikiwa kuna sababu ya muzuri yenye ilifanya ukose kualikwa. Mara nyingi, haiko hali fulani ndiyo inakufanya ujisikie kuwa peke yako, lakini ni mawazo yako ndiyo yanakufanya ujisikie hivyo.—Kanuni ya Biblia: Methali 15:15.

Usiwaze mubaya juu ya kila hali. Wakati unajisikia kuwa peke yako unaweza kuwaza hivi: ‘Hakuna siku mutu ananialika’ ao ‘kila mara watu wananiepuka.’ Lakini mawazo hayo yanaweza kukufanya ujisikie zaidi kuwa peke yako. Yanaweza kukufanya uendelee kuwa katika hali hii: Unajisikia kama wengine wanakutenga, hilo linakufanya ujitenge na wengine, na hilo linakufanya ujisikie kuwa peke yako, na hilo linakufanya tena ujisikie kama wengine wanakutenga.—Kanuni ya Biblia: Methali 18:1.

Ukuwe tayari kufanya urafiki na watu wenye miaka mingi kukupita. Biblia inaeleza juu ya maisha ya Daudi mwenye inawezekana alikuwa na miaka kati ya 13 na 19 wakati alimujua Yonathani. Yonathani alimupita Daudi miaka 30 . Daudi na Yonathani walikuwa na miaka tofauti, lakini walifikia kuwa marafiki wa sana. (1 Samweli 18:1) Unaweza pia kufanya hivyo katika maisha yako. Kijana mumoja mwanamuke mwenye miaka 21 anayeitwa Kiara anasema: “Hivi karibuni nimeanza kuona faida ya kuwa na marafiki wenye kuwa na miaka mingi kunipita. Niko na marafiki fulani wapendwa wenye kuwa na miaka mingi kunipita, na ninafurahia sana namna wanaona mambo kama watu wenye kukomaa na pia namna ni wenye kutulia.”—Kanuni ya Biblia: Ayubu 12:12.

Furahia faida za kuwa peke yako. Watu fulani wanajisikia kuwa peke yao kila mara wanapokuwa bila mutu mwengine. Lakini haupaswe kujisikia kuwa peke yako kwa sababu tu uko bila mutu mwengine. Kwa mufano, Yesu alifurahia sana kuwa pamoja na wengine, lakini alifurahia pia faida za kuwa peke yake. (Mathayo 14:23; Marko 1:35) Unaweza pia kufanya kama Yesu. Kuliko kuwaza kama kuwa peke yako ni jambo la mubaya, utumie wakati huo ili kufikiri juu ya baraka zenye umepata. Hilo linaweza kukufanya ukuwe rafiki muzuri kwa wengine.—Methali 13:20.

^ fu. 4 Majina fulani katika habari hii yamebadilishwa.