Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

MAMBO YENYE HISTORIA INATUFUNDISHA

Ignace Semmelweis

Ignace Semmelweis

IGNACE SEMMELWEIS ni jina lenye pengine halijulikane sana, lakini kazi yenye alifanya imeletea faida familia nyingi za leo. Alizaliwa katika muji wa Buda (leo unaitwa Budapest) katika inchi ya Hungaria. Alipata diploma yake ya kinganga kwenye Masomo ya Juu ya Vienna katika mwaka wa 1844. Wakati alikuwa mwalimu musaidizi kwenye hospitali kubwa ya kuzalisha ya Vienna katika mwaka wa 1846, Semmelweis alikutana na jambo lenye kuogopesha sana. Wanawake 13 juu ya 100 walikufa wakati wa kuzaa kwa sababu ya homa ya ambukizo la plasenta (fièvre puerpérale).

Mawazo mengi yalitolewa kuhusu jambo lenye lilileta ugonjwa huo, lakini hakuna hata wazo moja lenye lilisaidia. Mambo yote yenye walifanya ili kupunguza kifo, hayakuleta matokeo yoyote. Kwa sababu alihuzunishwa sana na kifo cha polepole na chenye maumivu makali cha wanawake wengi, Semmelweis aliamua kutafuta ni nini ilileta ugonjwa huo na namna ya kuuzuia.

Katika hospitali kwenye Semmelweis alikuwa anatumika, kulikuwa kliniki mbili za kuzalishia. Lakini jambo la kushangaza ni hili: katika kliniki ya kwanza hesabu ya wanawake wenye walikufa wakati wa kuzaa ilikuwa juu sana kuliko katika kliniki ya pili. Tofauti moja tu ni kwamba, wanafunzi wenye kujifunza mambo ya kinganga walifundishwa katika kliniki ya kwanza, na wanafunzi wenye kujifunza kuzalisha walifundishwa katika kliniki ya pili. Sasa, sababu gani tofauti hiyo? Wakati aliendelea kujiuliza ulizo hilo, Semmelweis alijifunza sana ili kujua sababu gani jambo hilo lilitokea, lakini hakujua kabisa ni nini ilitokeza kifo wakati wa kuzaa.

Katika mwanzo wa mwaka wa 1847, Semmelweis alifikia kujua ni nini kabisa ilitokeza ugonjwa huo. Jakob Kolletschka, rafiki yake mwenye alikuwa anatumika naye, alikufa kwa sababu damu yake iliambukizwa kisha kupata kidonda wakati alikuwa anachunguza maiti. Wakati alisoma ripoti ya uchunguzi wenye ulifanywa juu ya maiti ya Kolletschka, Semmelweis alitambua kama kulikuwa mambo fulani ya kufanana na mambo yenye yalipata wanawake wenye walikufa kwa sababu ya ambukizo la plasenta. Kwa hiyo, Semmelweis aliwaza kama pengine “sumu” yenye ilitoka kwenye maiti iliambukiza wagonjwa wenye kuwa na mimba na kuleta homa ya ambukizo la plasenta. Wanganga na wanafunzi wenye walijifunza mambo ya kinganga, wenye walizoea kuchunguza maiti mbele ya kuenda katika kliniki ya kuzalishia, bila kujua walikuwa wanaambukiza wanawake wenye mimba ugonjwa wakati wa kipimo ao wakati wa kuwazalisha! Hesabu ya wanawake wenye walikuwa wanakufa katika kliniki ya pili ilikuwa chini sana kwa sababu wale wenye walijifunza kuzalisha hawakuwa wanachunguza maiti.

Bila kukawia, Semmelweis aliweka sheria kali ya kunawa mikono kwa kutumia klorini mbele ya kufanya kipimo cha wanawake wenye mimba. Kulikuwa matokeo gani? Hesabu ya wanawake wenye walikufa wakati wa kuzaa ilishuka kutoka 18,27 juu ya 100 katika Mwezi wa 4 mupaka kufikia 0,19 juu ya 100 mwisho wa mwaka.

“Ninapenda kusaidia wanawake wasikuwe wanaogopa kuenda kwenye hospitali ili kuzaa, kusaidia bwana asimupoteze bibi yake na mama asimupoteze mutoto wake.”—Ignace Semmelweis.

Watu wote hawakufurahia matokeo ya muzuri yenye Semmelweis alipata. Matokeo yenye alipata yalifanya watu fulani wakuwe na mashaka juu ya mawazo ya mukubwa wake wa kazi kuhusu homa ya ambukizo la plasenta. Tena, mukubwa huyo aliona kama sheria yenye Semmelweis alitoa ilikuwa yenye kusumbua. Semmelweis alifikia kupoteza kazi yake katika muji wa Vienna na alirudia Hungaria. Katika inchi hiyo alisimamia kazi ya kuzalisha na kutunza wanawake wenye mimba kwenye Hospitali ya Saint Rochus katika muji wa Pest. Kwenye hospitali hiyo, namna yake ya kufanya kazi ilifanya hesabu ya wanawake wenye walikufa kwa sababu ya ambukizo la plasenta ishuke chini ya 1 juu ya 100.

Katika mwaka wa 1861, Semmelweis alichapisha kitabu The Cause, Concept, and Prophylaxis of Childbed Fever. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba watu walitambua faida ya mambo yenye alivumbua kisha miaka fulani. Katika miaka hiyo, watu wengi wenye wangeweza kupona walikufa sana.

Semmelweis alihakikisha kwamba sheria kuhusu usafi iliheshimiwa katika kliniki zenye alisimamia.—Muchoro wa Robert Thom

Semmelweis alifikia kujulikana kuwa mumoja kati ya watu wenye walianzisha ufundi mbalimbali wenye kujulikana leo wa kuua mikrobe yenye kuleta magonjwa. Kitabu chake kilisaidia kujua kama mikrobe inaweza kuleta ugonjwa. Yeye ni kati ya watu wenye walionyesha kama mikrobe inaweza kuleta ugonjwa. Mawazo yao yalionwa kuwa “muchango mukubwa sana katika mambo ya kinganga.” Jambo la kufurahisha ni kwamba, zaidi ya miaka 3000 mbele ya hapo, Sheria ya Musa, yenye kupatikana katika Biblia ilikuwa imetoa muongozo wenye kufaa juu ya maiti.